Serikali ya Hispania (Spain) imetangaza kumwita nyumbani balozi wake aliyekuwa akihudumu nchini Israel


 Serikali ya Hispania (Spain) imetangaza kumwita nyumbani balozi wake aliyekuwa akihudumu nchini Israel, hatua inayomaanisha kupungua kwa kiwango cha uwakilishi wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.


Kwa mujibu wa taarifa kutoka serikalini, ubalozi wa Spain uliopo katika mji wa Tel Aviv sasa utaongozwa na afisa wa muda (chargé d'affaires) badala ya balozi kamili. Hatua hiyo inaonyesha kuendelea kwa mvutano wa kidiplomasia kati ya mataifa hayo.


Mvutano huo umehusishwa na tofauti za misimamo kuhusu masuala ya Mashariki ya Kati, ikiwemo vita vya Gaza na hatua za kijeshi zinazohusisha Israel, Marekani, na Iran.


Spain imekuwa miongoni mwa nchi za Ulaya zilizokosoa vikali operesheni za kijeshi za Israel katika eneo hilo, jambo ambalo limechangia kuzorota kwa mahusiano kati ya pande hizo mbili.

Hatua ya kumwita balozi nyumbani ni ishara ya kidiplomasia inayotumika kuonyesha kutoridhishwa kwa nchi moja dhidi ya mwenendo wa nchi nyingine bila kuvunja kabisa uhusiano wa kidiplomasia.


Source: Reuters