Jeshi la Israel limeelezaa kuwa, Jeshi la Iran limetuma tena makombora ya masafa marefu kuelekea maeneo mbalimbali ndani ya Israel, hatua inayozidi kuongeza mvutano katika vita vinavyoendelea Mashariki ya Kati. Kwa mujibu wa taarifa ya jeshi hilo, mifumo ya ulinzi ya Israel iligundua mapema makombora hayo yakielekea nchini humo na kusababisha ving’ora vya tahadhari kusikika katika maeneo kadhaa ili kuwatahadharisha wananchi kuchukua hatua za kujilinda.
Jeshi la Israel pia limewataka wakazi wa maeneo yaliyo katika hatari kuacha shughuli zao mara moja na kuelekea kwenye makazi ya kujikinga dhidi ya mashambulizi ya anga, maarufu kama bomb shelters, hadi watakapotangaziwa kuwa ni salama kutoka. Tahadhari hizi hutolewa kila mara pale makombora au ndege zisizo na rubani zinapogunduliwa zikielekea nchini humo.
Aidha, jeshi hilo limeeleza kuwa mifumo ya kisasa ya ulinzi wa anga inaendelea kufanya kazi usiku na mchana ili kuzuia au kuharibu makombora hayo kabla hayajafika katika maeneo ya makazi ya raia. Baadhi ya makombora yanadaiwa kuzuiwa angani na mifumo ya ulinzi, huku vikosi vya uokoaji na usalama vikianza kufanya uchunguzi katika maeneo ambayo mabaki ya makombora yameonekana kuanguka.
Mashambulizi haya ni sehemu ya mfululizo wa mashambulizi ya kulipiza kisasi kati ya Iran kwa upande mmoja na Israel pamoja na Marekani kwa upande mwingine, baada ya mashambulizi ya pamoja yaliyofanywa dhidi ya malengo ya kijeshi ndani ya Iran. Tangu kuanza kwa mzozo huu mwishoni mwa Februari, Iran imerusha mamia ya makombora na ndege zisizo na rubani kuelekea Israel, huku pande zote zikiahidi kuendelea na mashambulizi zaidi.
Hali hii imeendelea kuongeza hofu duniani, huku nchi nyingi na mashirika ya kimataifa yakitoa wito wa kusitishwa kwa mapigano na kutafuta suluhisho la kidiplomasia ili kuzuia mzozo huo usitanuke na kuathiri usalama wa dunia nzima.

