
Donald Trump:Uingereza na Marekani sasa hauko kama ulivyokuwa zamani.
Donald Trump amesema kuwa Sir Keir Starmer “hajasaidia” na ameweka hatarini Uhusiano kati ya nchi hizo mbili baada ya kushindwa kuunga mkono vita yake dhidi ya Iran.
Rais huyo wa Marekani alisema ni jambo la kusikitisha sana kwamba uhusiano kati ya Uingereza na Marekani sasa hauko kama ulivyokuwa zamani.
Akimlaumu moja kwa moja Sir Keir, Bw. Trump alisema: “Hajasaidia. Sikuwahi kufikiria ningeona hilo. Sikuwahi kufikiria ningeona hilo kutoka kwa Uingereza. Tunaipenda Uingereza. Inasikitisha kuona kwamba uhusiano si kama ulivyokuwa”.
“Huu ulikuwa uhusiano imara kuliko yote. Na sasa tuna mahusiano yenye nguvu sana na nchi nyingine barani Ulaya”.
“Haitajalisha, lakini (Sir Keir) alipaswa kusaidia... alipaswa. Namaanisha, Ufaransa imekuwa nzuri. Wote wamekuwa wazuri. Uingereza imekuwa tofauti sana na wengine.”
Alidokeza pia kuwa huenda uamuzi wa Waziri Mkuu unatokana na kutaka kufurahisha wapiga kura wa Kiislamu, huku kiongozi huyo wa Labour akikosolewa kwa kile kilichoelezwa kama “kujifanya kushangaa” kufuatia mashambulizi ya Marekani dhidi ya Iran yaliyomwondoa Ayatollah Ali Khamenei.
Bw. Trump alisema ana ipenda Uingereza na watu wake, lakini akaongeza kuwa sasa si nchi inayotambulika kama ilivyokuwa zamani.
“Wazuieni watu wanaokuja kutoka mataifa ya kigeni wanaowachukia,” alimwambia Waziri Mkuu.
Ukosoaji wa Rais Trump dhidi ya Sir Keir umekuja wakati idadi ya wanajeshi wa Marekani waliouawa imefikia sita, huku Wamarekani wakihimizwa kuondoka katika nchi 15 za Mashariki ya Kati.
Iran imeshambulia ubalozi wa Marekani mjini Riyadh, Saudi Arabia, kwa kutumia ndege zisizo na rubani za kujitoa mhanga. Vyombo vya habari vya serikali ya Iran vimedai kuwa jengo la amri na uongozi katika kambi ya anga ya Marekani nchini Bahrain pia limeharibiwa.
Trump amesema jibu la kijeshi la Marekani kulipiza vifo vya Wamarekani pamoja na uharibifu wa ubalozi wake na kambi ya Bahrain liko karibu kutekelezwa, akionya kuwa mapigo makali zaidi yanakuja leo.
Israel pia imeanzisha mashambulizi mapya mjini Tehran na dhidi ya wanamgambo wa Hezbollah nchini Lebanon, ikituma pia wanajeshi wa ardhini asubuhi ya leo.
Keir Starmer ameshutumiwa kwa kudhoofisha Uhusiano Maalum kwa kutoruhusu ndege za kivita za Marekani kuanzisha mashambulizi yao dhidi ya Iran kutoka katika kambi za Uingereza huko Cyprus na Diego Garcia. Hata hivyo, ruhusa ilitolewa baadaye lakini kwa mashambulizi ya kujihami pekee.
Waziri Mkuu alisema jana kwamba alikuwa sahihi kuchelewesha uamuzi huo, akiliambia Bunge: “Rais Trump ameonyesha kutokubaliana na uamuzi wetu wa kutoshiriki katika mashambulizi ya awali, lakini ni wajibu wangu kuamua kilicho katika maslahi ya taifa la Uingereza. Hilo ndilo nimefanya, na ninasimama nalo.” Sir Keir alisema serikali yake “haiamini katika kubadilisha utawala kwa mashambulizi ya angani.”
Alipoulizwa kuhusu madai kwamba maamuzi ya kiongozi huyo wa Labour kuhusu Iran yanatokana na kutaka kufurahisha wapiga kura wa Kiislamu, Rais Trump alijibu leo: “Inawezekana.”
Chansela wa Duchy of Lancaster, Darren Jones, alisema leo kwamba mashambulizi ya awali ya Marekani na Israel nchini Iran hayakutimiza “vigezo vilivyowekwa na Waziri Mkuu.”
“Nimeyaona maneno ya Rais, lakini hayo hayaondoi ukweli kwamba tunafanya maamuzi kwa kuzingatia uhalali wa kisheria na maslahi ya Uingereza,” alisema waziri huyo wa Labour.
#iranisraelconflict #Bbcnews #dwkiswahili





