January: Lowassa aliisaidia CCM 2015
Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, January Makamba amesema uamuzi wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuondoka CCM, ulikuwa moja ya sababu ya chama hicho tawala kushinda urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana. Makamba pia amemshauri Lowassa kuachana na harakati za kuwania urais kwa kuwa ni muda mrefu tangu alipogombea kwa mara ya kwanza mwaka 1995 na kuishia kwenye uteuzi ndani ya CCM. “Kuondoka kwa Lowassa kwenda upinzani ndiyo kulirahisisha sisi (CCM) kushinda uchaguzi kwa sababu kuliwaondolea wapinzani hoja mbili muhimu ambazo ni ufisadi na mabadiliko,” alisema Makamba, ambaye alikuwa msemaji wa kampeni za CCM kwenye Uchaguzi Mkuu uliopita, wakati wa mahojiano na Mwananchi ofisini kwake Jumapili. Lowassa, ambaye alikuwa waziri mkuu wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Nne kabla ya kujiuzulu mwaka 2008 baada ya kuibuka kashfa ya Richmond, alijiengua CCM Julai 28, mwaka jana ikiwa ni siku chache baada ya jina lake kuchujwa pamoja na wagomb...