Iran imetoa rasmi majibu yake kwa pendekezo lenye vipengele 15 lililowasilishwa na Marekani Jumatano usiku, kwa mujibu wa chanzo kilichozungumza na chombo cha habari kutoka Iran,Tasnim.
Chanzo hicho kilisema kuwa majibu ya Iran yaliwasilishwa kupitia wapatanishi, na Tehran sasa inasubiri mrejesho.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, Iran imeweka wazi katika majibu yake kuwa vitendo vya uchokozi kama mauaji ya kulenga watu maalum lazima vikome. Pia imesisitiza haja ya kuweka masharti madhubuti ya kuhakikisha vita havijirudii tena, kulipwa fidia na gharama za vita, pamoja na kusitishwa kwa vita katika pande zote na kwa makundi yote ya upinzani yaliyoshiriki katika mapambano hayo katika eneo zima.
Chanzo hicho kiliongeza kuwa mamlaka ya Iran juu ya Mlango wa Hormuz ni haki yake ya kiasili na kisheria, na itaendelea kuwa hivyo.
Aidha, mamlaka hayo yanapaswa kutambuliwa kama dhamana ya utekelezaji wa makubaliano ya upande mwingine. Haya yote yametajwa kuwa ni masharti ya Iran, tofauti na madai yaliyotolewa wakati wa duru ya pili ya mazungumzo ya nyuklia mjini Geneva, yaliyofanyika siku chache kabla ya vita vya uchokozi vya Marekani na Israel mwezi Februari.
Chanzo kilisisitiza kuwa Iran inaona madai ya Marekani kuhusu mazungumzo kuwa ni “mradi wa tatu wa udanganyifu.” Kinasema kuwa Marekani inalenga malengo kadhaa kwa kujificha nyuma ya pazia la mazungumzo: kuipotosha dunia kwa kujionyesha kama inatafuta amani, kudhibiti bei ya mafuta duniani isishuke sana, na kununua muda ili kujiandaa na mashambulizi mapya ya kijeshi kusini mwa Iran.
Mwisho, chanzo hicho kilieleza kuwa kama Iran ilikuwa na mashaka kuhusu nia ya Marekani kuheshimu makubaliano kabla ya vita vya siku 12 vya Juni 2025, sasa ina mashaka makubwa zaidi kuhusu utayari wa Marekani kufanya mazungumzo kwa dhati. Kimeongeza kuwa wakati wa vita hivyo na hata sasa, Marekani imekuwa ikianzisha mashambulizi huku ikiendelea kudai kuwa iko kwenye mazungumzo, jambo linaloifanya Iran kuamini kuwa madai hayo yanatumika kuficha mipango ya uchokozi mpya.
