Nchi tatu za Afrika zimetajwa kwenye orodha ya nchi tano zilizokithiri kwa vitendo vya rushwa duniani katika ripoti ya Shirika la kimataifa Transparence iliyotolewa hivi karibuni.
Takwimu za Transparent International zilizotolewa mapema mwaka huu, zimeiweka Tanzania katika nafasi ya 117 duniani.
Miongoni mwa nchi tano zinazoongoza, mataifa ya Bara la Afrika, Somalia, Sudan na Sudan Kusini yametajwa. Somalia lililo katika pembe ya Afrika, ambayo imekuwa bila Serikali ya kitaifa tangu mwaka wa 1991, ndiyo taifa linaloongoza kwa ufisadi kwa kushika nafasi ya 167 ikifungana na Korea Kaskazini, Sudan Kusini likishika nafasi ya 163 kwa kufungana na Angola, Sudan ikiwa nafasi ya 165.
Nchi nyingine iliyo katika nafasi tano za juu kwa rushwa na ufisadi duniani ni Afghanistan iliyo na alama 166.
Katika ukanda ya Afrika Mashariki, Burundi inaongoza kwa kiwango cha juu rushwa na ufisadi ikiorodheshwa katika nafasi ya 150 duniani kwa kupata jumla ya alama 21.
Uganda na Kenya zimetoshana katika nafasi ya 139 zikiwa na alama 25 huku Tanzania ikipata alama 30.
Wakati Burundi ikitajwa kuongoza kwa rushwa Afrika Mashariki, Rwanda imetajwa ni taifa linaoongoza kwa kupiga vita ufisadi, ikiwa na alama 54 na kushika nafasi ya 44 kidunia.
Nchi ya Botswana iliyo kusini mwa Afrika, imeibuka kinara wa kupiga vita ufisadi ikipata alama 63.
Cape Verde ni ya pili ikiwa na alama 55, Shelisheli ya tatu ikiwa na alama 55, Rwanda ni ya nne, huku Mauritania ikiwa ya tano kwa kupata alama 53 na Namibia ikiwa katika nafasi ya sita kuwa na alama 53.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, nchi tano zenye kiwango kidogo cha rushwa na ufisadi duniani zinaongozwa na Denmark inayofuatiwa na Finland, Sweden ikiwa ya tatu, New Zealand na Uswisi imeshika nafasi ya tatno.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo nafasi ya kumi inashikiliwa na Uingereza ambayo imefungana na Ujerumani na Luxembourg zote zikiwa na pointi 81, huku Marekani na Australia zikiwa nafasi ya 16 kwa kutoshana pointi 96.
Ripoti hiyo imeonyesha katika nchi za Azerbaijan, Kazakhastan, Urusi na Uzbekistan, Serikali zimeminya uhuru wa vyombo vya habari pamoja na na taasisi za kiraia.
Urusi imepata alama ya 119 juu ya Azerbaijan, Guyana na Sierra Leone, ingawa imejitahidi kupanda kutoka nafasi ya 27 mwaka 2014 hadi ya 29 mwaka 2015.
Nchi ya Brazil, ambayo kampuni yake ya Petrobras inakabiliwa na kashfa kubwa ya rushwa, imeanguka kwa kiasi kikubwa kwa kiwango cha pointi tano na kupata alama 38 na imeshuka kwa nafasi saba hadi kufikia nafasi ya 76.
Mkuu wa Transparency International (TI), Jose Ugaz alikaririwa akisema, mlipuko wa ugonjwa wa ebola na kukithiri kwa mashambulizi ya kigaidi ni baadhi ya mambo yaliyosababisha kukithiri ufisadi barani Afrika.
“Haukuwa mwaka mzuri kwa mataifa ya Afrika hususan katika mataifa makubwa zaidi kiuchumi ya Nigeria na Afrika Kusini, ufisadi umesababisha kuibuka maandamano katika baadhi ya nchi vilevile mabadiliko ya kisiasa kutokana na chaguzi mkuu nchini Nigeria,” anasema na kuongeza:
“Ikiwa Afrika ina nia ya dhati kuondoa ubadhirifu wa mali za umma na matumizi mabaya ya mamlaka kwa faida binafsi, lazima zipige vita ufisadi.”
Hata hivyo, ripoti hiyo ya Transparence imeweka wazi kwamba Serikali nyingi za Afrika zinajaribu kupunguza vizuizi vya kufanya biashara, lakini wananchi wake bado hawajabadilika kimtazamo kuhusu maadili, ubadhirifu na ufisadi kwa viongozi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wachambuzi wa masuala ya kisiasa walisema Tanzania bado ina safari ndefu katika kupambana na rushwa na ufisadi na kwamba ni lazima ifanyike mikakati ya makusudi kumaliza tatizo hilo ikiwamo kuacha kuingia mikataba bila uwazi, wakisema ni aibu kwa taifa kuwa na mikataba mibovu.
Profesa Gaudence Mpangala wa Chuo Kikuu cha Ruaha anasema: “Tupo katika nchi zinazoongoza kwa rushwa. Kuwa nafasi ya 117 kidunia ni hali halisi, Rais John Magufuli ana kazi kubwa ya kufanya, sijui kama ataweza kupenya kwa vigogo. Nchi maskini kama Tanzania kuhusika kwa rushwa tutapata maendeleo kweli? Inasikitisha sana.”
Anasena: “Ingawa Rais Magufuli ameonyesha nia, zinahitajika juhudi za ziada, ili kasi aliyoanza nayo iendelee na aboreshe zaidi mikakati yake, asiishie kutumbua vijipu uchungu, bali atumbue na majipu makubwa kama la Escrow.”
“Tunataka tuwajue hao watu waliohusika, mbona hawakutajwa mpaka leo, huku Stanbic ikipigwa faini ndogo? Tunata kujua wazi waliohusika, wasiwasi wangu, majipu makubwa yatamshinda Rais Magufuli kuyatumbua,” anasema.
Profesa Abdallah Safari anaonyesha wasiwasi wake kuhusu ripoti hiyo ya Transparency akisema: “Hao wazungu hawana taarifa sahihi na yanayoendelea hapa nchini, ripoti ninayoiamini mpaka sasa ni ile ya Jaji Warioba na si nyingine yoyote.”
Anasema ripoti hiyo ilieleza kwa uwazi mianya ya rushwa ikiitaja Idara ya Mahakama kuhusuka na kwamba kwa uzoefu wake katika kazi za mahakamani bado hali hiyo ipo akisisitiza kwamba ripoti ya Jaji Warioba ndiyo inayotakiwa kufanyiwa kazi.
Desemba 7 mwaka 1997 Tume iliyoongozwa na Jaji Warioba kuchunguza rushwa nchini ilichapisha ripoti iliyoelezea mianya ya rushwa nchini kwa baadhi ya wafanyakazi wa umma kuchukua rushwa ili kujazia mishahara yao.
Ilibainisha pia rushwa kubwa iliyohusisha maofisa wa ngazi za juu na kutoa mapendekezo yaliyogusa takriban wizara na idara zote za Serikali.
Wakati Profesa Safari akisema hayo, Profesa Richard Mbuna anasema: “Kwa kweli sijapata muda wa kuipitia hii ripoti, ingawa kuna mtu ameniletea hapa. Kwa kifupi niseme inawezekana hao watafiti (TI), hawana taarifa za kutosha. Nchi hii ina kashfa nyingi nzito za rushwa, haikustaili kuwa hata ya 117, lakini pia labda kwa nchi za wenzetu, hali ni mbaya zaidi kuliko kwetu. Wakati sisi tunalia matatizo, kuna wenzetu wanalia zaidi ndiyo maana ripoti ikawa hivyo, nikiipitia nitakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuizungumzia zaidi kwa undani.”
Mwaka 2012 Tanzania ilishika nafasi ya 102 kwa rushwa duniani kati ya nchi 174 baada ya kupata alama 35.
Mwaka 2013, ilikuwa ya nchi ya 111 kwa alama 33, mwaka 2014 ikaporomoka hadi nafasi ya 119 baada ya kupata jumla ya alama31.
Swali linalobaki ni kwamba chini ya uongozi wa Rais Magufuli rushwa itaendelea kukithiri Tanzania au itapungua na kuthibitiwa?