SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Alhamisi, 28 Aprili 2016

T media news

Serikali Kununua Magari Mengi Zaidi ya Polisi


Serikali imepanga mwaka ujao wa fedha kununua magari  mengi kwa ajili ya kuyasambaza kwenye vituo tofauti vya Polisi nchini vyenye uhaba.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga alisema mpango huo utatekelezwa katika bajeti ya mwaka 2016/17.

Alisema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Igalula, Musa Ntimizi (CCM), aliyehoji kama wizara haioni umuhimu wa kuvipatia magari vituo vya polisi ambavyo havina magari katika jimbo hilo ili kurahisisha utendaji kazi.

Mbunge huyo pia alitaka wizara kumalizia ujenzi wa kituo cha polisi kikubwa kilichojengwa katika kata ya Loya halmashauri ya Tabora (Uyui) ambapo kwa sasa wananchi wameishiwa nguvu ya kuendeleza ujenzi huo.

Waziri alisema, serikali inatambua kazi kubwa inayofanywa na wananchi katika kuchangia maendeleo, alimtaka mbunge huyo kuwasiliana na wizara yake ili waweze kuona namna ya kusaidia kumalizia ujenzi wa kituo hicho ili kianze kufanya kazi.

Katika swali la msingi, mbunge huyo alitaka kufahamu ni lini kituo cha Loya kitafunguliwa hasa ikizingatiwa kuwa Loya ni zaidi ya kilomita 120 kutoka makao makuu ya Wilaya Isikizye ambapo ndiko kwenye kituo cha polisi.

Pia alihoji serikali ina mpango gani wa kuwaongezea bajeti ya mafuta kuwarahisishia watendaji kazi, maana maeneo ya jimbo ni makubwa na yote yanahitaji huduma za kipolisi.

Akijibu swali hilo, Kitwanga alisema pamoja na mwitikio wa wananchi na wadau kujenga kituo hicho, bado hakijakamilika sehemu ya kuhifadhi silaha, huduma ya choo na makazi ya askari.

Waziri huyo alisema, pindi hivyo vitu vitakapokamilika kituo hicho kitafunguliwa na askari watapelekwa.

Alisema, serikali ina mpango wa kuongeza bajeti ya mafuta katika maeneo mbalimbali kulingana na upatikanaji wa fedha, ili kukidhi mahitaji ya doria, misako na operesheni mbalimbali katika kutoa huduma ya ulinzi na usalama kwa wananchi.