MTUNZI:ENEA FAIDY
...Mama Eddy alitazama juu ili kuona kama kuna chochote lakini hakuona kitu. Ilimbidi atumie nguvu zake za uchawi alizokuwa Nazo ili kujilinda kwani aliziona dalili za kuvamiwa katika mazingira ya kutatanisha.
Mama Eddy ambaye jina lake halisi alijulikana kama Maimuna hakuwa Mtu wa kawaida Bali alitumwa na uongozi mkuu wa himaya aliyotokea Doreen ili kumsaidia kupata vitu alivyovihitaji.
Alitumia mbinu ya kujifanya mke wa Mr Aloyce ili kuweza kumteka vizuri na kumfanya asihangaike sana kuhusu mwanae kwani kulikuwa na uwezekano mkubwa sana wa kuharibu kazi. Maimuna alikuwa ni kijakazi mkongwe wa Bi Tatile na alikuwa akiaminika sana katika himaya ya Wanatatile kwani ni mtu pekee aliyewahi kufanikisha ajali kubwa ya mabasi mawili iliyoua abiria wote kisha wakafanywa kitoweo katika sikukuu ya kumpongeza Bi Tatile kama kiongozi bora wa wachawi wote Afrika Mashariki. Bi Maimuna alikuwa akiaminika sana kwa kila kazi anayoagizwa kwani hakuwahi kufanya makosa zaidi ya tukio moja tu la kuanguka kanisani akiwa katika harakati za kuwanga mchana.
"Maimuna! Maimuna! Hapa sio kwako na Leo ndio mwisho wa ubaya wako kwenye familia hii" ilisikika sauti nyororo isiyo na mkwaruzo hata kidogo huku ikijirudia rudia. Maimuna alibaki na mshangao wa ajabu sana, akataharuki huku akihema kwa nguvu. Akaaangaza macho kila upande pasipo kumuona mtu yeyote.
Akazidi kuchanganyikiwa sana. Ghafla wazo likamjia akilini mwake, bila kuchelewa akaamua kulifanyia kazi. Akanyoosha mkono wake wake wa kulia kisha nguvu nyingi zikamjia kama radi mkononi mwake. Bi Maimuna akaachia tabasamu mwanana akiamini hakuna kitakachomdhuru kwa wakati ule wala wakati mwingine wowote. akatulia kimya akimsubiri adui yake, lakini hakuona chochote zaidi ya ukimya mzito uliokuwa umetawala.
"Kumbe unaniogopa eeeh!" Alisema Maimuna.
"Ha ha ha! Sikuogopi Maimuna... Nakuvutia pumzi tu maana sina papara" sauti ile iliyojaa dharau ilisikika. Bi Maimuna hakutushika hata kidogo kwani alikuwa anajiamini kupita kiasi. Ghafla sura yake ikabadilika sana na kuwa sura ya kutisha sana.
Meno yakawa marefu kama mnyama mkali, kucha zikawa ndefu na Kali kama za chui anayemvamia swala, macho yake yakawa meusi huku mboni yake ikiwa nyekundu kama moto. Lengo lake lilikuwa ni kuonesha nguvu zake mbele ya adui yake ambaye hakujua ni nani. Ghafla kicheko kikali cha kutisha kilichojaa dhauri na jeuri kikasikika na kumfanya Maimuna ajione mdogo kama simimizi ilihali hamjui nana aliyemcheka.
Wakati huo huo Mlango ulifunguliwa na Mr Aloyce aliingia sebuleni pale.
"Mamaaaa" Mr Aloyce alipiga ukunga wa nguvu baada ya kumkuta mkewe akiwa na umbile la kutisha sana. Uvumilivu ulimshinda alijikuta anakimbia nje kama chizi huku akihema kwa nguvu. Mlinzi alimshangaa Mr Aloyce bila kuelewa kinachoendelea.
"Vipi bosi?" Aliuliza mlinzi huku akicheka sana. Mr Aloyce alianguka chini kama mzigo huku akihema kama Mtu aliyepanda mlima mrefu kwa kasi. Mlinzi alimsogelea na kumuuliza kilichojiri.
"Kuna maajabu humo ndani"
"Maajabu gani?"
"Mke.. Mke wangu...Ame..."
"Amefanyaje tena?" Aliuliza mlinzi kwa woga kwani alishapewa onto Kali na mwanamke yule kuwa asimfatilie kwa lolote. Lakini kabla hajasema chochote kuna kitu kiliwashtua Mr Aloyce na mlinzi wakabaki wameduwaa kwa mshangao.