SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumamosi, 18 Machi 2017

T media news

Yanga imeshindwa kusonga mbele michuano ya mabingwa Afrika


Dakika 90 za mchezo wa marudiano wa klabu bingwa Afrika kati ya Zanaco FC dhidi ya Yanga zimemalizika bila timu hizo kufungana na moja kwa moja Yanga imetupwa nje ya michuano hiyo mikubwa barani Afrika kwa ngazi ya vilabu.

Yanga imehukumiwa baada ya kuruhusu kufungwa goli kwenye uwanja wake wa nyumbani ambapo ililazimishwa sare ya goli 1-1 kwenye uwanja wa Taifa Jumamosi iliyopita.

Matokeo hayo yanaifanya Yanga kuangukia kwenye michuano ya Confederation Cup na kuiacha Zanaco ikifuzu katika hatua ya makundi ya Caf Champions League 2017.

Msimu uliopita Yanga ikiwa chini ya Hans van der Pluijm, ilifuzu hatua ya makundi ya michuano ya Confederation Cup baada ya kuondoshwa kwenye michuano ya Caf Champions League.

Yanga ilihitaji ushindi wa aina yoyote au sare ya kuanzia magoli 2-2 ili isonge mbele kwenye hatua inayofata lakini imeshindwa kufanya hivyo na kujikuta ikiondoshwa kwenye michuano hiyo baada ya sare tasa kwenye mechi ya marudiano.

Zanaco wamefaidika na goli la ugenini walilopata kwenye mechi yao ya jijini Dar es Salaam na kuizuia Yanga kupata goli kwenye ardhi ya Zambia.

Kesho Jumapili March 19, 2017 wawakilishi wa Tanzania kwenye michuano ya kombe la shirikisho Afrika Azam FC itakuwa ugenini Swazland ikicheza mechi ya marudiano dhidi ya Mbabane Swallows. Mechi ya kwanza kwenye uwanja wa Azam Complex Azam ilipata ushindi wa goli 1-0.