SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 6 Desemba 2017

T media news

EDA NI NINI? NA NANI ANAKAA EDA?‎

BISMILLAH.‎

Eda ni muhula maalum ambao mwanamke, aliyekwisha olewa, anatakiwa ‎kusalia bila ya kuolewa wala ‎kuposwa kutokana na  mojawapo wa sababu ‎mbili kuu: ‎
‎A. kutalikiwa\kuachwa au kuachika na ‎
B. Kufiwa na mumewe (au mume kutoweka ‎au kukimbia pasipo kujulikana ‎aliko…).  ‎

Kwa maana hiyo, Eda ni muhula wa wajibu, uliofaradhishwa ndani ya ‎Qur’ani ‎Tukufu na Hadithi za Mtume ‎ﷺ‎ ambazo ziko nyingi. ‎Mwenyezi ‎Mungu anasema: ‎
‏ وَالْمُطَلَّقَاتُ يَتَرَبَّصْنَ بِأَنفُسِهِنَّ ثَلاَثَةَ قُرُوَءٍ وَلاَ يَحِلُّ لَهُنَّ أَن يَكْتُمْنَ مَا خَلَقَ اللّهُ فِي أَرْحَامِهِنَّ )‏
‏ . وقوله تعالى ‏‏(وَالَّذِينَ يُتَوَفَّوْنَ مِنكُمْ وَيَذَرُونَ أَزْوَاجاً يَتَرَبَّصْنَ بِأَنفُسِهِنَّ أَرْبَعَةَ أَشْهُرٍ وَعَشْراً )‏
‎“Na wanawake walioachwa (watalikiwa):  wangoje (wasiolewe)  mpaka ‎tohara tatu ‎zishe. Wala haiwajuzii kuficha mimba aliyoumba Mwenyezi ‎Mungu katika ‎matumbo yao, ikiwa wanamuamini Mwenyezi Mungu na siku ‎ya Mwisho”.Q;2.28.‎

‎“Na wale wanaofiwa na waume zao, miongoni mwenu na kuacha wake, wake ‎hao ‎wangoje (wakae eda) miezi mine na siku kumi.” Q.2:34.‎

Ama mja mzito aliyefiwa na mumewe, basi eda yake ni tokea tarehe ya ‎kufa ‎mumewe hadi ajifungue. ‎
Vivyo hivyo, mtalikiwa mja mzito, eda yake ni hadi kujifungua. ‎
Akijifungua tu basi eda yake imeisha.‎
‏‎(‎وَأُوْلَاتُ الْأَحْمَالِ أَجَلُهُنَّ أَن يَضَعْنَ حَمْلَهُنَّ‏‎ ).‎
‎“Na wale waja wazito, basi muhula wao ni pale watapotua ujauzito wao.”‎

Ama mwanamke alieachwa kabla ya kujamiiana na mumewe, yeye hakai ‎eda ‎yoyote, na wala hana mahari –iwapo mahari hayo hayakutajwa ‎kinaganaga-, ‎isipokuwa  kiliwazo (i.e. kiacha nyumba, yaani kitu cha kuanzia ‎maisha ya ujane). ‎

Lakini ikiwa kima cha mahari kilishatajwa na akaachwa kabla ya kujamiana ‎na ‎mumewe, basi mwanamke huyo, pamoja na kwamba hakai eda, anapaswa ‎kulipwa ‎nusu ya mahari ya kima kilichotajwa; ila kama yeye mwenyewe au ‎walii wake ‎‎(mzee wake, kwa mwanamwari) atasamehe malipo hayo Q.2;37.  ‎Na katika aya ‎nyengine Q.33.49 Mwenyezi Mungu anasema:  ‎
‏‎ (‎يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نَكَحْتُمُ الْمُؤْمِنَاتِ ثُمَّ طَلَّقْتُمُوهُنَّ مِن قَبْلِ أَن تَمَسُّوهُنَّ فَمَا لَكُمْ عَلَيْهِنَّ مِنْ عِدَّةٍ ‏تَعْتَدُّونَهَا ‏فَمَتِّعُوهُنَّ وَسَرِّحُوهُنَّ سَرَاحاً جَمِيلاً‎ )‎
‎“ Enyi mlioamini! Mtakapowaoa wanawame; wenye kuamini kisha mkawpa ‎talaka ‎kabla ya kuwagusa (kuingiliana kimwili), basi hamna eda juu yao ‎mtakayoihisabu. ‎Na wapeni cha kuwaliwaza na muwawache muachano ‎mzuri” Q.33.49.‎

Ama mwanamke anayefiwa na mume basi eda yake ni miezi mine na siku ‎kumi, ‎kama nilivyotaja hapo juu na kunakili aya ya Qur áni.  Na ni sawa ‎ikiwa mume ‎huyo alikwisha jamiiana na mkewe au la; mke atakaa eda ya ‎miezi mine na siku ‎kumi. ‎Yaani, mfiwa na mume anakaa eda ya miezi mine na ‎siku kumi. Iwapo ana mimba basi mpaka ajifungue.‎

Vile vile, mke huyo anamrithi mumewe huyo aliyefariki, awe aliingiliana ‎naye ‎kimwili au la. Kama mume hakuacha mtoto au watoto (kwa mke ‎mwengine, kwa ‎mfano) basi mwanamke atarithi robo ya mali yote ya mume ‎na kama mume aliacha ‎mtoto au watoto basi mke atarithi thumuni (one ‎eighth) ya mali yote ya mume.  ‎

Hivyo ndivyo alivyoamua Mtume ‎ﷺ‎  kwa Sahaba mmoja aliyekuwa ‎akiitwa: ‎Ma’qal Ibn Yasar ambaye alifariki na kuacha mke kabla ya kuingiliana ‎naye ‎kimwili. ‎

Hali kadhalika, Ibn Masúd – mmoja wa Maswahaba wakubwa- alikabiliwa na ‎kesi ‎kama hiyo ya mke kufiwa na mume ambaye bado hajaingiliana naye ‎kimwili. Ibn ‎Mas’ud akatoa fatwa ya mke kukaa Eda na pia kumrithi ‎mumewe. Akapewa ‎khabari kuwa Mtume ‎ﷺ‎  alitoa hukumu kama hiyo kwa ‎Ma’qal Ibn ‎Yasar! Ibn Mas’ud alifurahi sana kuona kuwa hukumu yake ‎imewiana na hukumu ‎ya Mtume ‎ﷺ‎ . ‎

Pili, ni muhimu kujua kwamba mwanamke anakaa eda kwenye nyumba ‎ya ‎mumewe, awe mume yuhai au la, na katika muhula wote wa eda, ‎mwanamke huyo ‎anaendelea kulishwa kama kawaida kuktokana na mali ya ‎mume, mpaka eda yake ‎ishe.  Mwenyezi Mungu anasema: ‎

‎(‎لَا تُخْرِجُوهُنَّ مِنْ بُيُوتِهِنَّ وَلَا يَخْرُجْنَ إِلَّا أَنْ يَأْتِينَ بِفَاحِشَةٍ مُبَيِّنَةٍ‎ ) ‎الطلاق/1‏
‎“….Msiwatoe katika nyumba zao wala asitoke wenyewe, ila wakifanya jambo ‎la ‎ufasiqi ulio wazi. Na hii ni mipaka ya Mwenyezi Mungu. Na anayekiuka ‎mipaka ya ‎Mwenayezi Mungu basi amejidhulumu nafsi yake. Hujui; (sababu ‎ya kuamrishw ‎hwaha): huenda Mwenyezi Mungu akazusha jambo jingine ‎baad ya haya (yaani ‎jambo la kupatana).” Q.65:2.‎

HEKIMA YA EDA.‎

Hakuna halali ambayo anaichukia Mwenyezi Mungu kama anavyochukia ‎talaka. ‎

Hii ni kwa sababu ndoa ni fungamanisho takatifu,, ni ahadi tu ya mdomo ‎anayotoa mtu, mbele ya watu, kuwa ‎yeye anafunga ndoa na fulani kwa JINA ‎LA MWENYEZI MUNGU. Jina la ‎Mwenyezi Mungu ndilo linalotumika ‎kumtoa mtoto wa watu katika familia yake na ‎kumuingiza katika familia ‎nyengine kabisa. Hivyo, si jambo la kupendeza hata ‎kidogo, bali ni jambo ‎analolichukia Mwenyezi Mungu kumuona mja wake ‎aliyetumia Jina la ‎Mwenyezi Mungu kumuoa binti fulani na baadaye anaivunja ndoa ‎hiyo na ‎kumuacha! Anachukia Mwenyezi Mungu. ‎

Lakini wakati huo huo, watu wawili wakeshaoana na ikafika hadi kuwa ‎hawawezi ‎kuvumiliana na kuishi pamoja basi hakuna haja ya kuwalazimisha ‎kuishi maisha ya ‎mateso na chuki na uhasama. Inakuwa, kwa wote wawili, ‎kama wako jela katika ‎nyumba yao ya ndoa! Hivyo basi,  Kama walivyooana ‎kwa salama na maelewano, ‎wanatakiwa waachane kwa salama na maelewano; ‎bila ya chuki, uhasama au ‎dhuluma. Na ili kutoa nafasi ya kuja kutambua ‎kuwa uamuzi haukuwa wa busara, ‎au kwamba yumkini: mwanamke ana uja ‎uzito, jambo ambalo ni jukumu la mume ‎kumkimu na kumtunza, na kwa ‎jamii kutambua kuwa mtoto atayezaliwa ni mtoto ‎wa ndoa, basi ndipo ‎pakawekwa muhula wa eda.  Hivyo, tunaweza kusema kuwa ‎hekima za eda ni ‎nyingi. Miongoni mwake ni:-‎

a)‎ Kutoa fursa ya kutafakari na kupima kwa walioachana, ili waweze ‎kurudiana ‎bila ya kufung ndoa tena.‎

b)‎ Kujua kama fuko la uzazi lina mwana au la, na hivyo kulinda nasaba na ‎koo ‎na kuepuka kuchanganya vizazi visivyo husiana kidamu.‎

c)‎ Kutunza na kuendeleza haki za urithi, kwa mujibu wa Quráni na Sunna ‎za ‎Mtume ‎ﷺ‎ ‎

d)‎ Kuisaidia jamii katika kujua na kutambua nasaba za koo ndani ya jamii, ‎na ‎hivyo kujua nani ana jukumu lipi, kabla ya jamii yenyewe kubeba ‎jukumu ‎kama hilo iwapo hakuna wa kulibeba.‎

e)‎ Kutambua jukumu la utunzaji na kukimu familia analo nani? Yaani ‎mume ‎jukumu lake haliishi hadi pale itapojulikana wazi wazi kuwa hakuna ‎kizazi ‎chochote kati yake na aliyemuacha.‎

f)‎ Kuwapa fursa wazazi na jamaa wa pande zote mbili kutafuta suluhu ya ‎ndoa ‎ya watoto au jamaa zao.‎

g)‎ Kumpa fursa mwanamke aliyefiwa na mumewe kuwaliwaza wakwe zake ‎na ‎familia ya marehemu mume wake.‎

h)‎ Kulipa uzito unaostahiki fungamanisho la ndoa katika jamii.‎

i)‎ Kuonesha kuwa talaka si jambo la mchezo, mtu kuoa na kuacha tu, ‎akidhani ‎hana majukumu na dhamana hata baada ya kuacha.‎
Na mengi mengi mengine, ambayo haiwezekani kuyataja yote hapa.‎

والله أعلم

وبالله التوفيق

السيد عبد القادر شريف آل الشيخ أبى بكر بن سالم‎ ‎

Imejbiwa na Sayyid Abdulqadir Shareef

NI RUHUSA KUNUKUU, kama ilivyo, pasi na kubadilisha au kuongeza ‎chchote, na kuweka kwenye FB yako au kwenye ‎WhatsApp na kwenye ‎Makundi ya Mitandao ya Kijamii za Kiislamu, ‎kwa lengo la kusambaza na ‎kuelimisha Dini. Changia kusambaza ‎Dini, ujipatie thawabu.‎