SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumanne, 12 Septemba 2017

T media news

Katibu Mkuu CHADEMA Asimulia Jinsi Tundu Lissu Alivyo Vunjwavunjwa kwa Risasi

Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Vincent Mashinji amesema mwanasheria mkuu wa chama hicho, Tundu Lissu ameumizwa vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake na kwamba alipigwa risasi nyingi tofauti na risasi tano zilizoelezwa.

Dk Mashinji amesema Lissu amevunjwa miguu yake, nyonga na mkono wa kushoto, jambo ambalo linawapa madaktari kazi kubwa na kuimarisha afya yake.

Kiongozi huyo amesema jana asubuhi Lissu alianza kusumbuliwa na kifua, jambo lililowalazimu madaktari kumwekea mashine za kumsaidia kupumua, hata hivyo anasema walizitoa baadaye na leo Jumanne ameamka salama.

"Bado najisikia uzito wa kuelezea jamii ya Watanzania hali ya kiongozi wetu Tundu Lissu, najua nina jukumu kubwa kama mtendaji wa chama kutaarifu umma juu ya hali ya Lissu inavyoendelea. Ni majonzi makubwa sana na kama kuna mtu katika taifa hili alifanya hicho kitendo anatakiwa ajitafakari sana. Mpaka jana asubuhi ameenza kupatwa na matatizo ya kifua kutokana na kulala kitandani muda mrefu, na kwa sababu mguu wake wa kulia umevunjwa vunjwa kwa risasi, nyonga yake pia mkono wake umevunjwa kwa risasi lakini 'inshallah' kama nilivyosema awali kuwa Mwenyezi Mungu ndiye anayeamua kuchukua roho ya nani na aache ya nani", amesema Mashinji..

Amesema Lissu ameongezewa damu nyingi akiwa Dodoma na bado anaendelea kuongezewa huko Nairobi. Amesema madaktari wanajitahidi kuokoa maisha yake na kwamba ana imani kwamba watafanikiwa.

"Waswahili wanasema hujafa hujaumbika, kwa kweli wamemuumiza kwa hiyo ndugu zangu hiyo hali ya Lissu jana ilikuwa mbaya mpaka wakamuwekea mipira ya kupumulia lakini ilipofika wakati wa mchana hali yake ilikuwa inaendelea vizuri. Tunasafari ndefu ya kuhakikisha Lissu anapona, sasa hivi wamemtibu zile sehemu za ndani ambazo zingeweza kuhatarisha maisha yake kwa zile risasi zilizopita tumboni na sehemu nyingine", amesema Mashinji.
 

"Mhe. Lissu ni kweli tuliambiwa alipigwa risasi tano katika mwili wake lakini kulingana na hali ya mwili ulivyobomolewa yawezekana zilizidi. Leo ni siku ya tano akiwa anatibiwa hospitali na mpaka sasa hivi ameshafanyiwa oparesheni tatu nadhani itabidi kuzisitisha kidogo ili kumpa ahueni aweze kupumzika na yeye. Tulitegemea ingekuwa suala la kawaida tu yeye kwenda kutibiwa na kurudi lakini imekuwa tofauti. Msilie wala kusononeka kwa sababu Lissu bado yupo hai anaendelea kupigana na sisi, kuhakikisha kwamba anapona na kurudi kuendeleza ukombozi Watanzania ili kufikia uhuru wa kweli na mabadiliko ya kweli", amesisitiza Mashinji.

Kwa upande mwingine, Mashinji amesema wanajiandaa kisaikolojia kumpokea Lissu na hali ambayo atarudi nayo kwa kuwa hiyo ndiyo zawadi waliyopewa na Mwenyezi Mungu.