SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatatu, 4 Septemba 2017

T media news

Hakimu Atoa Siku 14 kwa Pande Mbili Kuwasilisha Hoja Katika Kesi ya Lissu ya 'Dikteta Uchwara

Upande wa mashtaka umeieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa imefunga ushahidi katika kesi ya ‘Dikteta Uchwara’ inayomkabili Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu.

Wakili wa Serikali, Mutalemwa Kishenyi amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Godfrey Mwambapa kuwa kesi hiyo imeitishwa kwa ajili ya ushahidi, lakini wamemaliza ushahidi.

Baada ya kueleza hayo, Lissu amesema Wakili wake Peter Kibatala hayupo, isipokuwa anawasilisha hoja kwamba hana kesi ya kujibu ambapo hata hivyo, Wakili Kishenyi amedai kuwa hakuna kipengele kinachoruhusu mshtakiwa kusema hana kesi ya kujibu ama la.

Kutokana na hatua hiyo, Lissu amedai kuwa hoja za upande wa mashtaka sio sahihi, kwa sababu kifungu cha 230 cha Mwenendo wa Makosa ya Jinai kinatoa nafasi kueleza kama kuna kesi ya kujibu ama la akisema

”Hivyo, tunaomba tupate fursa kwamba kwa ushahidi uliopo katika record hakuna kesi ya kujibu.”

Hata hivyo, Wakili Kishenyi alidai kuwa anasisitiza kwamba hakuna kifungu cha namna hiyo, hivyo Mahakama itoe uamuzi kama ana kesi ya kujibu ama la.

Kutokana na mvutano huo, Hakimu Mwambapa amesema anakubaliana na hoja za upande wa mashtaka kwamba hakuna kifungu kinachomruhusu mshtakiwa kueleza kama ana kesi ya kujibu ama la, isipokuwa ana haki ya kuieleza Mahakama.

Hakimu Mwambapa amesema anatoa siku 14 kwa pande zote mbili kuwasilisha hoja zao September 18, 2017 na October 4, 2017 atatoa uamuzi kama mshtakiwa ana kesi ya kujibu ama la.