SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Alhamisi, 16 Februari 2017

T media news

Wema Sepetu Adai Mashabiki Walimpa Nguvu Alipopata Matatizo.

Siku chache baada ya kuachiwa kwa dhamana mwigizaji wa filamu, Wema Sepetu amedai maombi kutoka kwa mashabiki na watu mbalimbali yalimsaidia kumpa nguvu alipokuwa mahabusu katika sakata la dawa za kulevya lililohusisha watu mbalimbali wakiwamo wasanii.

Kupitia ukusara wake wa Instagram, Wema alisema alipitia kipindi kigumu kwenye maisha na dua pekee ndizo zilizomsaidia kukabiliana na ugumu huo.

“Najua wengi mlikuwa mnaniombea, nashukuru kwa sala na dua zenu kwani zimenisaidia kwa kunipa nguvu wakati nikiwa kwenye wakati mgumu katika maisha yangu.

“Napenda kuwashukuru mashabiki wangu wote duniani kwa kuniamini na kusimama kwa kipindi chote hiki, pia napenda kuwashukuru wasanii wenzangu wote,” anasema.

Wema aliandika: “Asante sana mwanasheria wangu, Alberto Msando kwa kunisimamia na kuwa na mimi bega kwa bega wakati huu mgumu. Nakuombea kwa Mungu akupe moyo huohuo wa kuwatetea wanyonge.”

Mwigizaji huyo ambaye aliwahi kushika taji la Miss Tanzania mwaka 2006, pia alimshukuru Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Nnape Nnauye.

Vilevile, Wema aliandika ujumbe mzito uliosomeka: “Unaweza kukutana na vikwazo, lakini usikubali kushindwa, hata hivyo lazima ukutane na vikwazo ili ujijue wewe ni nani na kwa namna gani unaweza kutoka kwenye vikwazo hivyo.”