SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Alhamisi, 3 Novemba 2016

T media news

TANESCO Yaanza Mchakato Wa Kupeleka Umeme Kiwanda Cha Bakhressa Kama Ilivyoagizwa Na Rais Magufuli.


Na: Frank Shija & Daud Manongi, MAELEZO.

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) limeanza kutekeleza agizo la Rais Dkt. John Pombe Magufu la kufikisha umeme kwenye kiwanda cha kusindika matunda cha Bakhressa Food Product kilichopo Mwandege mkoani Pwani.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Kaimu Meneja Uhusiano wa Tanesco Makao Makuu, Leila Muhaji amesema kuwa agizo hilo limeshaanza kutekelezwa katika hatua mbalimbali na kuahidi kuwa litakamilika kwa wakati.

Muhaji amaesema kuwa agizo linapotolewa na Mhe. Rais kinachobaki ni utekelezaji tu, hivyo kufuatia agizo hilo Tanesco wameanza kufanya utekelezaji kwa kuchukua hatua kadhaa ili kuhakikisha wanakamilisha kulingana na wakati kama agizo linavyosema.

“Utekelezaji wa agizo la Mhe. Rais unaendelea na hadi kufikia mwezi Desemba tutakuwa tumefikisha umeme katika kiwanda hicho”. Alisema Bi. Muhaja.

Aidha alitumia fursa kutoa rai kwa uongozi wa kiwanda hicho kuanza uzalishaji punde umeme utakapofika kiwandani hapo ili kuongeza uzalishaji.

Kwa upande wake Meneja Ushirikiano wa Jamii wa Kiwanda cha Bakhressa Food Product Hussein Sufian Ally amesema kuwa wanamshukuru Rais Dkt. Magufuli kwa kuona umuhimu wa kupelekewa umeme kiwandani hapo.

Aliongeza kuwa utekelezwaji wa agizo hilo utakapo kamilika utasaidia kuongeza uzalishaji na kupunguza gharama ambazo kwa sasa zinachangiwa na matumizi ya Jenereta katika kuendeshea uzalishaji wa Kiwanda hicho.

Utekelezaji huu umefutia agizo la Rais alilolitoa tarehe 06/10/2016 wakati wa uzinduzi wa Kiwanda cha kusindika matunda cha Bakhressa Food Product ambapo alimuagiza meneja wa Tanesco Mkoa wa Pwani kuhakikisha ndani ya miezi miwili umeme uwe umefika kiwandani hapo