SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumamosi, 6 Agosti 2016

T media news

Hatimaye Tundu Lissu Aachiwa Kwa Dhamana Baada ya Mvutano Mkali wa Kisheria

Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA Mhe. Tundu Lissu alipewa dhamana saa tatu usiku wa kuamkia leo  katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, baada ya kukana mashitaka matatu ya uchochezi aliyosomewa.

Lissu alitimiza masharti ya dhamana baada ya mvutano mkali wa zaidi ya saa 5 na kujidhamini mwenyewe kwa dhamana ya shilingi milioni 10, na kesi yake imeahirishwa hadi Agost 19, 2016.

Mapema jana Katika Mahakama ya Hakimu MkazI Kisutu, ulinzi uliimalishwa tangu saa mbili asubuhi ambapo askari polisi waliokuwa na silaha walikuwa wakizunguka huku na huko kuhakikisha wafuasi wa chama hicho hawakusanyiki katika eneo la mahakama, huku kukiwa na matarajio ya kuwa wakati wowote atafikishwa mahakamani hapo.

Viongozi mbalimbali wa chama hicho nao walikuwepo katika mahakama hiyo kufuatilia kesi hiyo ya Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki.

Majira ya saa nane mchana Mhe Lissu alifikishwa mahakamani na kupandishwa kizimbani.

Akisomewa Mashataka na Wakili wa Serikali Paul Kaduche mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Cyprian Mkahe ilielezwa kuwa Mhe Tundu Lissu alifanya makosa hayo matatu Agost 2 mwaka huu, katika maeneo ya mahakama hiyo, kwa kutoa maneno ya uchochezi, maeneno ya dharau katika mfumo wa utoaji haki pamoja na kuidharau mahakama ya Kisutu.

Mshtakiwa alikana mashtaka hayo na baadaye ukatokea mvutano mkali wa kisheria juu ya uhalali wa dhamanaambapo mawakili wa serikali walikuwa wakipinga mtuhumiwa huyo kupewa dhamana.

Baada ya mvutano wa zaidi ya saa 5, kuanzia saa 10 jioni hadi saa tatu usiku,  hakimu alikubali hoja za upande wa utetezi na kutoa dhamana baada ya Lissu kukamilisha masharti ya dhamana hiyo.

Mara baada ya kuchiwa, Lissu akiongozana na baadhi ya viongozi wa chama chake, aliondoka mara moja mahakamani hapo.