SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Alhamisi, 7 Aprili 2016

T media news

KUELEKEA MECHI NA AL AHLY,MURO AWAPIGIA MAGOTI SIMBA

DAR ES SALAAM


YANGA imewaomba mashabiki wa Simba na Azam kuwaunga mkono katika mchezo wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly utakaochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam keshokutwa.

Akizungumza Dar es Salaam, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Yanga, Jerry Muro alisema ni muhimu mashabiki hao kuwaunga mkono katika mchezo huo wa kimataifa na kuelekeza utaifa mbele.

“Wenzetu Watunisia wamekuwa wakiungana hasa timu zao zinapocheza na timu za nje. Tunaomba Azam na Simba waje tushirikiane kutafuta mafanikio ya kuhakikisha tunaing’oa Al Ahly,” alisema.

Alisema imefika wakati wakabadilika na kuweka kasumba nyuma, hivyo mabadiliko hayo yameanzia kwao wakiamini bila kuwa kitu kimoja hawawezi kufika mbali. Kuhusu maandalizi yao, alisema wanaendelea vizuri na kambi yao ya Pemba na kwamba wamedhamiria kuing’oa Al Ahly ili kutimiza ndoto zao za kufikia hatua ya makundi.


                                                                    

Alisema iwapo watafanikiwa kuifunga timu hiyo ambayo iliwasili Dar es Salaam jana alfajiri uwezekano wa kuwa mabingwa wa Afrika utakuwepo na kusisitiza kuwa ushindi dhidi ya Al Ahly unatakiwa uanzie kwa mashabiki pia.

Aidha alitaja viingilio vya mchezo huo kuwa ni Sh 5,000 kwa viti vya kijani na bluu, viti vya rangi ya chungwa ni Sh 7,000, VIP B na C ni Sh 25,000 wakati VIP A ni Sh 30,000.