SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumanne, 15 Agosti 2017

T media news

Madaktari wa Serikali Wanaojiongezea Kipato Kwenye Hospitali Binafsi Kukiona...

Serikali inatarajia kutoa mikataba ya uwajibikaji kwa waganga wakuu wa mikoa, wilaya na waganga wafawidhi wa hospitali zote nchini ifikapo mwezi ujao na ambayo itadhibiti wale wanaojikita zaidi katika hospitali binafsi kwa ajili ya kutafuta kipato cha ziada.

Kwa mujibu wa mikataba hiyo, daktari atakayeshindwa kufikia malengo atakuwa amejiachisha kazi mwenyewe.

Akizungumza na Nipashe juzi, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Dk. Zainabu Chaula, alisema lengo la mikataba hiyo kwa waganga wakuu wa mikoa, wilaya na waganga wafawidhi wa hospitali ni kuboresha huduma za afya kwa kuwa haziridhishi.

“Huu mkataba utakuwa ni kwa kila mwaka, lakini sio wa kutishana na wala sio jambo jipya ni la kawaida… tunachotaka ni uwajibishaji,” alisema Dk. Chaula.

“Tunatamani uanze kutolewa Septemba mwaka huu (mwezi ujao), hivyo tutawaita, ili kuwajulisha kuhusiana na hili kwa kuwa kutakuwa na kikao mwezi huu.”

Dk. Chaula alisema kwa madaktari wanaofanya kazi katika vituo vingine vya afya huku majukumu yao waliyopangiwa na serikali wakiyaacha watadhibitiwa na mkataba huo.

“Hapo ndipo tutaondoana,” alisema Naibu Katibu Mkuu (Tamisemi) huyo. “Mtu anaacha kuona wagonjwa, anaenda kwenye kliniki yake (binafsi) anapata pesa na huku nako anadai fedha.”

“Mimi nimesomea udaktari (na) ninafanya kazi zangu kwa uadilifu, nilitamani wote wawe kama mimi.

“Sasa mtu akienda kinyume siwezi kumuacha.

“Tunachokitaka ni huduma za afya ziwe bora.”

Dk. Chaula alisema mkataba huo umeshaandaliwa kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, isipokuwa kuna baadhi ya vipengele vya kufanyia maboresho.

“System (mfumo) ya (wa) mkataba huo ni hivi… mimi nafanya kazi na Katibu Mkuu ndiye anayeniangalia utendaji wangu, Katibu Mkuu anakuwa na Waziri,” alisema Dk. Chaula.

“Mkurugenzi wa Tamisemi atakuwa karibu na waganga wakuu wa mikoa 26. Sasa mganga mkuu wa mikoa anaingia mkataba na waganga wakuu wa wilaya; hivyo kila mtu anamshika mwenzake.

“Hivyo mganga mkuu wa mkoa hawezi kukubali kuangushwa na mganga mkuu wa wilaya.

“Mfano waziri ameibua jambo kwenye halmashauri hapo anayewajibika ni mganga mkuu wa mkoa (kwamba) kwa nini hajawajibika?”

Alisema lengo la mkataba huo ni kila mmoja kutimiza wajibu wake bila kutumwa na kutakiwa kujitathmini mwenyewe.

“Mimi nimeteuliwa kwenye eneo la afya hivyo siridhiki na huduma, natamani ziwe nzuri (na), ili ziweze kuwa nzuri tukaona tupeane mikataba, ili kila mtu atimize majukumu yake,” alisema zaidi Dk. Chaula.

“Ndiyo maana tunataka kuwekeana malengo mahususi nikikuambia uniletee taarifa tarehe tano, ni lazima niipate tarehe tano. Usipoileta ina maana utakuwa una shida.
“Yaani nikitaka kitu fulani kikamilike kwa wakati na wewe hujafanya hivyo ina maana hujawajibika.

“Ifike wakati ukiona hujafanya vizuri katika nafasi yako uone hiyo nafasi hustahili, utajiengua mwenyewe… huko ndipo tunakoelekea.”

Dk. Chaula alisema kuwekwa kwa mkataba huo kutasaidia kupatikana kwa mabadiliko katika huduma za afya, ambayo kwa sasa hayawezi kuonekana kwa kuwa hali ilikuwa tete.

“Huu mkataba ni kila mwaka.

“Yaani kwenye mwaka wa fedha tunasimama na kuangalia je, umetimiza majukumu yako? Kama hujakamilisha majukumu yako utashuka, mwingine atapanda.”

MKATABA MWINGINE
Mganga Mkuu wa Mkoa mmoja ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini alieleza Nipashe kuwa suala hilo la mkataba lilijadiliwa katika mkutano mkuu wa mwaka wa Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya uliofanyika mkoani Dodoma mwezi uliopita.

Alisema wametakiwa kufanya kazi kwa malengo na kuonyesha mikakati ambayo wataitekeleza katika kipindi hicho, hivyo kama daktari hatofanya vizuri, uwezekano wa kupatiwa mkataba mwingine ni vigumu.

“Sisi kila siku tunatakiwa kufanya kazi kwa malengo,” alisema.

“Kwa mfano unasema mimi kwa safari hii nitahakikisha vituo kadhaa vinakamilika, nitahakikisha kutakuwa na upatikanaji wa dawa kwa asilimia 100, ndio malengo yenyewe ambayo tunajiwekea.”

Alisema mfumo huo umepitishwa katika mkutano huo kwa ajili ya watendaji wote – waganga wafawidhi wa hospitali, waganga wakuu wa wilaya pamoja na wa mikoa.
Alisema kwa sasa wanasubiri maelekezo ya serikali namna ambavyo watasaini mkataba huo.

“Tunangoja maelekezo namna ambavyo tutasaini (maana) kwa mfano mimi kama mganga mkuu wa mkoa, naingia mkataba na mganga mkuu wa wilaya,” alisema.

“Lengo la serikali ni kuona huduma za afya zinakuwa bora; yule atakayeshindwa kutekeleza mikakati yake hatapatiwa mkataba (mpya).”

Alisema jambo hilo ni nzuri, tatizo lipo kwa watendaji wavivu wanaoweza kuuchukia mfumo huo.

“Serikali ya sasa inataka tufanye kazi kwa kujituma na kuweka uzalendo mbele kwa wale wanaofanya kazi kwa kusuasua ama wale wenye mikataba na hospitali nyingine wanaweza kuuchukia huo mfumo ila kwa mimi sioni kama kuna tatizo,” alisema.

Chanzo: Nipashe

Mytake:
Ukiona mwenzio ananyolewa wewe tia maji , udaktari usio na mipaka kwaheri !