SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatatu, 26 Desemba 2016

T media news

Askofu: Kataeni kutoa mimba

ASKOFU Mkuu wa Jimbo la Bukoba, Desiderius Rwoma katika ibada ya mkesha wa Krismasi alikemea vitendo vya utoaji mimba.

"Kataeni kutoa mimba, hao watoto wanahitaji kuwa hai."

Pia aliwataka Wakristo kuthamini ufukara na umaskini kwa sababu ndio ambao Kristo alichagua kuzaliwa kwao na sio kwa matajiri. Alisema utajiri ni muda tu na vitu vya kupita.

Alisema Krismasi pia iwe fundisho la watu kuwa wanyenyekevu na kutojiona kama wanastahili kupewa kila jambo.

"Nashauri pokea kwa unyenyekevu ushauri wa wazazi wako, ushauri wa viongozi wako na ushauri wa walimu wako."

Kiongozi huyo pia alitoa mwito kwa Watanzania kuwaheshimu wanawake,

"Tuna utamaduni wa kuheshimu First Lady (mke wa Rais) lakini napenda niwaambie kwamba Bikira Maria ni zaidi ya First Lady, naombeni tumheshimu mwanamke huyu."

Wakati huohuo, Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Frederick Shoo ameitaka serikali kuichunguza upya pombe aina ya kiroba na ikiwezekana iondolewe sokoni.

Askofu Dk Shoo aliyasema hayo jana katika salamu zake za Krismasi kwa Wakristo wote nchini. Akisoma salamu hizo kwa niaba ya Askofu Shoo, Mchungaji wa Kanisa la Kiinjili Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Usharika wa Muhimbili, Leah Mwakenja alisema vijana wengi ambao ni nguvu kazi ya taifa wanatumia pombe hiyo ya kiroba na kushindwa kufanya kazi kwa kuwa wanalewa wakati wa kazi.

Alisema suala la kilevi aina ya kiroba ni kero kwa vijana kwa kuwa wamekuwa wakifanya kazi wakiwa wamelewa au kuwa navyo mifukoni hasa madereva wa pikipiki, daladala na wapiga debe na kusababisha ajali kila uchwao na wengine kupoteza maisha.

"Vijana wanakunywa kiroba nyakati za kazi, wengine hulegea na kudhoofu mwili huku wengine wakifanya matendo kama vichaa, ni vema serikali ikakipima upya na kupiga marufuku uuzwaji wa kilevi hicho, na kukiondosha sokoni."

Ilisema sehemu ya tarifa hiyo ya Askofu Dk Shoo. Alisema kiroba imekuwa janga na serikali isipochukua hatua za haraka za makusudi basi taifa litaangamia kwa kupoteza nguvu kazi ambao ni taifa la kesho.

Wakati huo huo, Askofu Mkuu Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Dk Alex Malasusa leo ataongoza ibada maalumu ya makanisa yote ya Protestanti (CCCT) itakayofanyika Kanisa la AIC Chang'ombe. Ibada hiyo itaanza saa nane kamili mchana ikisindikizwa na vikundi mbali mbali vya kwaya.

Katika hatua nyingine, ibada ya misa ya shukrani kwa makanisa yote nchini imepangwa kufanyika Januari 8 kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja.