Klabu ya Yanga imethibitisha kuwa Hans Van der Pluijm amekubali kuwa Mkurugenzi wa Ufundi wa klabu hiyo huku nafasi ya Kocha Mkuu ikichukuliwa na George Lwandamina kutoka Zesco ya Zambia.
Hans Van der Pluijm
Akithibitisha taarifa hizo, Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo Clement Sanga amesema uongozi wa klabu hiyo ulikuwa kwenye mazungumzo na kocha Hans ili aridhie maamuzi hayo, na hatimaye amekubali kufanya kazi na kocha George Lwandamina.
Akizungumzia nafasi ya kocha msaidizi Juma Mwambusi, Sanga amesema hatma yake bado haijafahamika kwa kuwa nafasi ya kocha msaidizi itategemea matakwa ya kocha mkuu, na kwamba mambo yote yatakapokaa sawa, uongozi utatoa taarifa rasmi kwa vyombo vya habari kwa ajili ya kulitambulisha rasmi benchi jipya la ufundi.
Kuhusu baadhi ya wachezaji kuachwa kutokana na mapendekezo ya kocha huyo mpya, Sanga amesema kuwa hilo halijawa wazi na kwamba hadi sasa hawajapokea mapendekezo yoyote ya kuacha wachezaji na kinachosubiriwa kwanza ni ripoti ya mwalimu Hans ya mzunguko wa kwanza wa ligi.
Clement Sanga
"Tunatarajia kupokea ripoti ya mwalimu muda wowote kuanzia leo, tutaijadili na baada ya hapo tutamkabidhi kocha mpya halafu ndiyo tutajua kama kuna wachezaji atataka kuwaacha au la" Amesema Sanga
Akifafanua sababu za mabadiliko hayo Sanga amesema kuwa uamuzi huo ni kwa ajili ya kuboresha kikosi hicho, na kwamba ni mabadiliko ya kawaida katika uendeshaji vilabu.