SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumapili, 17 Septemba 2017

T media news

Serikali yawaonya Wakuu wa Wilaya kwa kuweka watu rumande

Na. Atley Kuni- TAMISEMI- Dodoma.

Wakuu wa wilaya na Wakurugenzi wa Mamlaka za serikali za Mitaa, kutoka katika mikoa minane hapa nchini wameiahidi serikali ya awamu ya tano inayo ongozwa na Mh. Dkt. John Pombe Magufuli makubwa mara baara yakumalizika kwa mafunzo ya siku tano yaliyoendeshwa na Taasisi ya Uongozi Institute  kwa lengo lakuwaimarisha watendaji hao wakuu katika ngazi ya Wilaya na Halmashauri katika majukumu yao ya kila siku.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mjini, Josephine Matiro, amesema mafunzo hayo yaliyowashirikisha jumla ya washiriki 84 kati ya 89 waliokuwa wahudhurie yamewakumbusha majukumu yao lakini kuwaongezea uzoefu kutokana na wao kutoka maeneo tofauti tofauti.

“Tulivyokuja sio tunavyoondoka, miongoni mwetu tulikuwa tunagombana katika maeneo yetu sisi na wakurugenzi lakini kupitia semina hii, tunaondoka tukiwa tumepatana” alisema Matiko na kuongeza,

“Naibu Waziri sisi tuahidi kwamba, tunakwenda kubadilika kwani mafunzo haya yamekuwa na manufaa makubwa, labda tuombe jambo moja mafunzo haya yawe ya mara kwa mara, kwa kuwa yanasaidia hata kupungua Pressure na stress za kukaa kituoni kwa muda mrefu, tunapokutana hivi inatusaidia kubadilishana uzoefu.

Naibu waziri  Selemani Jafo.

Akifunga mafunzo hayo, Naibu Waziri wa Nchi Tawala za Mikoa na Serikali Mitaa, Selemani Jafo, amewataka wakuu hao wa Wilaya na Wakurugenzi, kuacha kuingiliana katika utendaji badala yake wazingatie mipaka ya kazi inayowaongoza.

Mipaka ya kazi.

“Wakuu wa Wilaya ninyi mpo kwa ajili yakumwakilisha Rais katika maeneo yenu, hivyo msifanye Interference badala yake mkafanye intrevession, Wataalam na mkurugenzi wakishaamua kama mkuu wa Wilaya vema mkashauriana kwa hoja na kukubaliana kwa misingi yakujenga na sio kubomoa.”

Kero za Wananchi

Jafo amewataka Viongozi hao kwenda kusimamia sheria, taratibu na kanuni bila ya kumuonea mtu, huku akwasisitiza kwenda kujenga nidhamu na kutatua kero za wananchi ili kero zinazofikishwa ngazi ya Wizara zikomee huko huko kwa kuwa katika ngazi ya Wilaya na Halmashauri wapo wataalam wengi hivyo ametaka wataalam hao watumike vema. “Matatizo yatakayowashinda basi vema mkayafikisha katika Ngazi ya mkoa, sio kuwaacha wananchi wanalipa nauli zao kupeleka kero Wizarani” alisema Jafo

Vita ya Dawa zakulevya na Rushwa

Naibu Waziri Jafo hakuacha kuwahimiza viongozi hao kwenda kupambana na dawa za kulevya katika maeneo yao, “Kapambaneni na vita dhidi ya dawa za kulevya, tunafahamu dawa za kulevya zimekuwa mwiba mchungu kwa nguvu kazi ya Taifa, tukailinde nguvu kazi hii na agenda hii iwe ya kudumu katika vikao vyenu vyote vya maamuzi. Aidha adui rushwa msimuache akastawi katika maeneo yenu, haiwezekani mgonjwa akakosa bomba la sindano.”

Makusanyo kwa njia ya kieletroniki

Naibu Waziri Selemani Jafo amewaagiza wakurugenzi kukusanya mapato kwa njia ya mifumo ya kieletroniki na kuonya wale wote wanaofanya diversion ya mifumo iliwarudi kwenye njia za kizamani, “Jiji la Dar es Salaam leo, nimpongeze sana dada yangu Zipolla, amekuwa mfano wa kuigwa kutoka Mil. 15 hadi Mil 600 ya makusanyo ya ushuri wa maegesho ambapo hapo awali wengine walishindwa hii ni hatua yakupigiwa mfano, ajenda ya mapato iwe yetu sote.”

Usimamizi wa Rasilimali na thamani ya fedha.

“Lazima (value for Money) katika miradi yetu yote mkaipe kipaumbele, jana nimetoa maelekezo yamekwenda tayari juu ya ukarabati wa Vituo 172 vya afya nchini kote kwa kuwa fedha hizo nimeelekeza mtumie force Account,  niseme ule msemo wa vijana wa mtaani, {Kipa katoka},  kazi kwenu lakini ifikapo Desemba 30, 2017 kazi hiyo iwe imekamilika, alisema Jafo na kuongeza kuwa, “Tulifanya vema katika shule kwenye zile Bil 25 leo watoto wote wapo shule, tukafanye vizuri pia katika hili la Vituo vya afya”.

Mwisho Naibu Waziri Jafo hakuacha kuwaonya Viongozi hao dhidi ya matumizi mabaya ya  sheria inayowaruhusu kuamuru kumuweka mtu rumande kwa saa 48, “sheria hii ipo lakini itumike kunapo sababu sio kuitumia kiholela” alisema Mh. Jafo.

Salaam za Uongozi Institute

Akitoa salaama za Uongozi Institute Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo, Kadai Singo, alisema mambo makubwa wanayotazamia mara baada ya mafunzo hayo ni pamoja na weledi, mbadiliko, wilaya zibadilike lakini kupata mrejesho wa matokeo chanya baada ya mafunzo kukamilika.

Salaam za TAMISEMI na Dkt. Zainabu Chaula

Awali akitoa taarifa fupi juu ya mwenendo wa mafunzo kabla yakumkaribisha Naibu Waziri kufunga mafunzo hayo Naibu Katibu Mkuu Afya wa TAMISEMI, Dkt. Zainabu Chaula alisema, “Mara baada yakukamilika kwa mafunzo hayo yaha shabaha ya Wizara ni kuwapatia mafunzo ya aina hii Wakuu wa Mikoa ili katika utendaji wakawe na uelewa wa pamoja”, Dkt. Chaula alimueleza Naibu Waziri aliyefika kufunga mafunzo hayo.

Mikoa ambayo wakuu wa wilaya wamepatiwa mafunzo hayo katika awamu hii ilikuwa ni  Shinyanga, Mbeya, Rukwa, na Ruvuma, Mikoa mingine ni  Songwe, Dar es Salaam, Njombe na Iringa.

Selemani Jafo, alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tano kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mikoa minane kwenye ukumbi wa Hazina Mjini Dodoma.

Selemani Jafo, alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tano kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mikoa minane kwenye ukumbi wa Hazina Mjini Dodoma huku Wakiwa wanamsikiliza kwa makini.

Josephine Matiro Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga akitoa neon la Shukrani mara baada yakufungwa kwa mafunzo hayo.

Bibi Zainabu Chaula, Naibu Katibu Mkuu Afya TAMISEMI, alipokuwa akitoa neon kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufunga Semina hiyo


Baadhi ya Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya wakisikiliza kwa makini Hotuba ya Ufungaji wa Semina hiyo ya siku tano. (Picha zote na Idara ya Habari Maelezo- Dodoma)