SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumanne, 5 Septemba 2017

T media news

Serikali Kuwarudisha Kwao Raia Watatu wa China.....

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt Kebwe Stephen Kebwe, ameagiza kukamatwa mara moja na kurejeshwa nchini mwao raia watatu wa China wanaodaiwa kuwepo nchini bila kibali na kuendesha shughuli za uchimbaji wa madini katika eneo la Maseyu Morogoro.

Dkt Kebwe ametoa maagizo hayo jana Septemba 3 kufuatia maagizo aliyopewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alipokuwa mkoani humo ambapo alimtaka RC na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa kwenda katika Kijiji cha Maseyu kufuatilia utendaji wa kampuni ya Zhong Fenq kama inafuata sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Waziri Mkuu alitoa maagizo hayo wakati akizungumza na viongozi na watumishi wa Kiwanda cha Philp Morris kinachotengeneza sigara aina ya Marlboro akiwa katika ziara yake ya kukagua maendeleo ya viwanda mkoani Morogoro.

Agizo hilo limefuatia malalamiko ya Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Omary Mgumba kuwa wawekezaji hao kutoka China wanaendesha shughuli za uchimbaji wa mabo katika kijiji cha Maseyu wilayani Morogoro bila ya kuwa na kibali.

Mgumba alisema tangu mwaka 2011 wawekezaji hao wameendesha shughuli zao bila kulipa kodi za Serikali na tozo za Halmashauri, hivyo kuikosesha Serikali mapato.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu katika kijiji cha Maseyu kuna Wachina wa kampini ya Zhong Fenq wanachimba mabo na hawana kibali na hakuna kodi yoyote wanayolipa Serikalini tangu mwaka 2010 walipoanza uzalishaji.”

Mbunge huyo ambaye machimbo hayo yako jimboni kwake aliongeza kwamba licha ya uongozi wa mkoa kwenda katika eneo hilo na kuizuia kampuni kuendelea na uchimbaji hadi itakapopata vibali walikaidi na kuendelea na shughuli.

Waziri Mkuu amesema hakuna muwekezaji anayeruhusiwa kufanya kazi bila ya kufuata sheria, kanuni na taratibu za nchi. Hivyo ameagiza kesho Mkuu wa Mkoa afuatilie Wachina hao na kuona namna gani wamezingatia sheria za nchi.

Alisema iwapo watabaini kwamba wawekezaji hao hawajafuata sheria, kanuni na taratibu hatua zichukuliwe dhidi yao ikiwa ni pamoja na kuwaondoa katika eneo hilo chini ya ulinzi na kuwasiliana na ubalozi wa China Nchini.

Baada ya Mkuu wa Mkoa  wa Morogoro kubaini ukweli katika hilo, ametoa amri raia hao kukamatwa mara moja na kurejeshwa nchini China kutokana na kukiuka za kiukwekezaji ikiwamo kuishi na kufanyakazi nchini bila vibali.

Pia Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa watu wote wenye nia ya kutaka kuwekeza katika miradi mbalimbali nchini Tanzania kuhakikisha wanafuata sheria, kanuni na taratibu za uwekezaji.