SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumanne, 19 Septemba 2017

T media news

Kichuya: Nitakuwa mfungaji bora msimu huu

Na Zainabu Rajabu

WINGA machachari wa Simba, Shiza Ramadhani Kichuya amewaeleza mashabiki wa timu hiyo kuwa wavumilivu kutokana na kucheza michezo yote mitatu ya ligi kuu msimu huu bila kupachika bao lolote.

Kichuya ambaye msimu uliopita alimaliza msimu akiwa na mabao 12, alikuwa tegemeo katika ufungaji kikosini hapo lakini hivi sasa bado hajacheka na nyavu.

Kutokana na ukame huo wa mabao, tayari mashabiki wa Simba wameanza kuhoji juu ya ukame huo.

Kichuya amesema: “Wawe wavumilivu naamini bado nina uwezo wa kufunga, kwa sasa ligi bado ni mbichi sana na pia hao waliotangulia kufunga naamini nitawapita kwa juhudi zangu na hatimaye kuwa mfungaji bora.”

Mbali na hilo, Kichuya aliongezea kuwa mechi zao za Kanda ya Ziwa huwa ni ngumu sana kutoka na wapinzani wao kuwakamia lakini wanaamini wataondoka na alama tatu ili kushika nafasi ya kwanza katika msimamo wa Ligi kuu.

Alhamisi hii Simba watakutana na Mbao FC ya jijini Mwanza katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini humo.

Simba wataingia uwanjani hapo wakiwa na kumbukumbu ya ushindi wa mabao 3-2 walioupata msimu uliopita dhidi ya wenyeji wao hao.