SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Ijumaa, 15 Septemba 2017

T media news

Jeshi la Polisi Makao Makuu na TCRA Wazungumzia Makosa ya Mtandaoni na Hatua Ambazo Mwananchi Anatakiwa Kuchukua


Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini Kamishina Msaidizi wa Polisi (ACP) Barnabas Mwakalukwa amewataka wananchi kwa ujumla wanaofanyiwa vitendo vya uhalifu mitandaoni wasiende TCRA bali wanapaswa kutoa taarifa katika jeshi la polisi.

ACP Mwakalukwa amebainisha hayo wakati alipokuwa anazungumza katika mkutano wa pamoja na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuhusu suala zima la uhalifu wa makosa ya mitandao ambapo kwa sasa limeshika kasi kubwa

"Chochote kinachofanyika ambacho ni kosa jinai nawaomba msiende Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), kwa watoa huduma wa mitandao ya simu mbalimbali wala katika vyombo vya kutolea habari bali unapaswa uje katika kituo cha polisi utoe taarifa zako kama ni kosa la jinai kwa sababu mkienda huko uchunguzi utakuwa shida kwa maana wewe mwenyewe utaweza kusababisha hata yule aliyekutendea uhalifu atoroke", amesema ACP Mwakalukwa na kuongeza;

"Kutokana na kukua kwa teknolojia vitu vingi vimekuwa vikifanyika 'online' kwa hiyo hii mitandao ya kijamii imeonekana ni muhimu sana kwenye maendeleo, lakini pia imebadilisha mbinu ya kufanya uhalifu katika mitandao ya kijamii kwa kutumiwa na baadhi ya watu kutapeli, hata kutishia kuua, hivyo jeshi la polisi limejipanga kwa ajili ya kushughulikia makosa ambayo yanatokana na mtandao", amesema Mwakalukwa.

Kwa upande wake,Kaimu Mkurugenzi wa TCRA, Thadayo Ringo amesema analishukuru jeshi la polisi kwa kuweza kuwasaidia katika kuwatatulia changamoto mbalimbali hasa za kiusalama huku akiwataka wananchi watakaopata matatizo katika mtandao kwenda kutoa taarifa polisi ili waweze kuwasaidia kabla ya kufika kwao.