SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatatu, 4 Septemba 2017

T media news

Exclusive: Erasto Nyoni ametaja sababu iliyomfanya akashangilie goli kwenye picha ya marehemu Mafisango

Erasto Nyoni alifunga goli lake la kwanza kwenye msimu mpya wa ligi (2017/2018) huku akiwa na jezi ya Simba, kumbuka ilikuwa siku ya ufunguzi wa ligi kuu Tanzania bara August 26, 2017 ambapo Ruvu Shooting walinyanyasika kwa kufungwa bao 7-0.

Nyoni siku hiyo alicheza kama beki wa kushoto wa Simba, Nyoni ndio alifunga goli la sita dakika ya 81. Baada ya kufunga goli hilo, Nyoni alikwenda moja kwa moja kwenye bango lenye picha ya marehemu Patrick Mafisango na kuionesha picha hiyo.

Mafisango aliwahi kuichezea Simba huku akitajwa kuwa miongoni mwa wachezaji wa kigeni waliofanya vizuri katika klabu hiyo katika eneo la kiungo. Mafisango alifariki May 17, 2012 kwa ajali ya gari.

Shaffihdauda.co.tz ikaamua kumtafuta Nyoni kutaka kujua ni kwa nini aliamua kwenda kushangilia kwenye picha ya Mafisango? Alikuwa anamaanisha nini ili watu wengine wapate kujua.

“Kifo cha Mafisango kilinihuzunisha sana, jamaa alikuwa mtu safi sana hakuna mtu ambaye amewahi kuniambia aliwahi kuwa na matatizo na Mafisango tangu nimemfahamu,” Erasto Nyoni.

Urafiki wa Nyoni na Mafisango

“Unajua watu wengi hawajui kuwa mimi na Mafisango tulikuwa marafiki sana kabla ya kukutana Azam FC, tulifahamiana wakati mimi nacheza Burundi (Vital’O) yeye akiwa Rwanda. Tulikuwa tunakutana kwenye mechi za kirafiki za vilabu vyetu huko ndio tulianza kuwa marafiki.”

“Baadae mimi nikarudi Tanzania nikajiunga na Azam, kama bahati Mafisango akasajiliwa na Azam tukawa wachezaji wa timu mmoja. Urafiki ukazidi kukua tukawa ndugu kabisa tunasaidia kwenye mambo yetu mbalimbali. Hata alipoondoka Azam na kujiunga na Simba bado tuliendelea kuwa karibu sana.”

Haikuwa bahati mbaya kwenda kwenda kwenye picha ya Mafisango, alijipanga

“Kabla mechi haijaanza nililiona bango la mashabiki likiwa na picha ya maremu Mafisango, ghafla nikamkumbuka sana. Nikaomba Mungu kwamba endapo ikitokea nikafunga goli kwenye ule mchezo basi nitaenda kushangilia kwenye picha ya Mafisango. Bahati nzuri Mungu akafanikisha nikafunga ndio maana niakenda kwenye picha ya Mafisango.”

Alikuwa anamaanisha nini kwenye picha ya Mafisango? 

“Ni ishara ya kumuenzi na heshima kwake, hakuna mtu ambaye hajui kazi ya Mafisango uwanjani kwa hiyo kwa upande wangu niliamua kwenda kutoa heshima kwa rafiki yangu kipenzi.”

Klabu ya Simba imeamua kumuenzi marehemu Mafisango kwa kuistaafisha jezi namba 30 ambayo ilikuwa ikivaliwa na Mafisango mchezaji wa kimatafa wa Rwanda aliyezaliwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.