SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatatu, 8 Mei 2017

T media news

Jengo la Yanga kupigwa mnada

HUKU jengo lake la Jangwani likiwa hatarini kupigwa mnada kutokana na deni la zaidi ya Sh. milioni 300, imebainika Klabu ya Yanga inaandamwa na balaa jingine baada ya kutajwa kwenye orodha ya wadaiwa sugu wa Shirikisho la Soka (TFF).

Klabu hiyo ya jijini Dar es Salaam inadaiwa Sh. milioni 62.9 na shirikisho hilo ambazo hazijulikani zilitokana na huduma ipi, hata hivyo.

Kwa mujibu wa ripoti ya ukaguzi wa hesabu za fedha za TFF iliyotolewa Januari 19, mwaka jana na Kampuni ya Ukaguzi ya TAC, mbali na Yanga kuna wadaiwa sugu wengine 17 ambao kwa pamoja wanatakiwa kulilipa shirikisho hilo jumla ya Sh. milioni 301.394.

Wadaiwa hao ni pamoja na aliyekuwa Katibu Mkuu wa kilichokuwa Chama cha Soka Tanzania (FAT sasa TFF), Michael Wambura anayedaiwa Sh. milioni 50.828 na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo inayodaiwa Sh. milioni 157.408.

Wengine ni Creastus Ruta Sh. milioni 10.781 na Chama cha Soka Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) Sh. milioni 8.213, Jumbe Magati Sh. milioni 1.954, aliyekuwa Ofisa wa Habari wa TFF, Florian Kaijage Sh. milioni 1.88, Simba Technology Sh. milioni 1.5 na Asheri Gasabile Sh. milioni 1.408.

Pia wamo Adam Brown Sh. milioni 1.093, Ramadhani Kilemile Sh. 900,000, Chama cha Soka Wilaya ya Ilala (IDFA) Sh. 880,000, aliyekuwa Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu (TPLB), Silas Mwakibinga Sh. 875,770, Katibu Mkuu wa zamani wa TFF, Fredrick Mwakalebela Sh. 468,000, Ahmed Naheka Sh. 414,652, Edith Ruben Sh. 295,000, Glory Mwenda Sh. 150,000 na Raymond Wawa Sh. 132,252.

Ripoti hiyo ya ukaguzi inaonyesha kuwa, wadau hao wa soka wanadaiwa kiasi hicho cha fedha na TFF kwa kipindi cha kuanzia miaka mitatu hadi nane kutoka tarehe ya ripoti ya ukaguzi (Januari 19, 2016).