SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 15 Februari 2017

T media news

KISWAHILI LUGHA INAYOKUA KWA KASI DUNIANI

Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imeanza kutekeleza malengo iliyojiwekea ya kuifanya Lugha ya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani ili iweze kupata soko na kutumika duniani kote katika kurahisisha mawasiliano ya watumiaji wa lugha hiyo.

Rai hiyo imetolewa na Waziri mwenye dhamana ya Sekta na Utamaduni Mhe. Nape Moses Nnauye alipokua akizungumza na wadau wa Sekta hiyo jana Jijini Dar es Salaam.

“Tumejipanga kuangalia changamoto zinazotokana na Sera na Sheria tulizonazo, changamoto za kirasilimali na mambo ya kiutashi kwani kwa kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo Kiswahili kitaendelea kuwa bidhaa ambayo itavuka mipaka ya nchi na kuitangaza nchi yetu” amesema Mhe. Nnauye.

Akizungumza wakati wa Mkutano huo Katibu Mtendaji Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) Dkt. Selemani Sewangi amewataka waandishi wa vitabu vya Kiswahili kuzingatia weledi wa matumizi fasaha ya lugha ya Kiswahili wakati wa uandishi wa vitabu ili kuweza kuisaidia jamii hasa mashuleni kujua misamiati fasaha ya lugha hiyo.

Kwa upande wake mdau wa Utamaduni nchini Dkt. Musa Hans ameiomba serikali kuhamasisha wageni wote wanaoingia nchini kujifunza lugha ya Kiswahili na kuandaa mwongozo kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu utakaowataka watoto wote wanaoingia sekondari kuwa na kamusi za Kiswahili na kamusi za Kiswahili Kingereza zitakazowasaidia kujua misamihati ya lugha ya Kiswahili.

Naye Mdau wa Utamaduni mama Mipango ameipongeza serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuendelea kutafuta njia mbalimbali za kueneza na kukuza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya nchi.

Katika kuendeleza ukuaji wa Lugha ya Kiswahili Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amekua mstari wa mbele kutumia lugha ya Kiswahili katika shughuli mbalimbali za kiserikali kama vile Mkutano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Mkutano wa Umoja wa Afrika (AU) ambapo kwa kufanya hivyo lugha hii imeweza kusambaa kwa kasi zaidi.

 Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye akizungumza na wadau wa sekta ya Utamaduni walipokutana nao Jijini Dar es Salaam kujadili namna ya kukifanya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani na kukisambaza nje ya mipaka ya nchi.

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Annastazia Wambura (katikati) akichangia wakati wa majadiliano jana  Jijini Dar es Salaam na wadau wa Sekta ya Utamaduni katika kukuza na kukifanya kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani. Kushoto ni Waziri wa Habari Mhe. Nape Moses Nnauye na kulia ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Bibi. Nuru Millao

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na wadau wa Sekta ya Utamaduni (hawapo pichani) walipokutana jana Jijini Dar es Salaam kujadili namna ya kukifanya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani ndani na nje ya nchi.

: Baadhi ya Wadau wa Sekta ya Utamaduni wakifuatilia kwa makini hoja zilizokua zikiendelea wakati wa majadiliano na viongozi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kujadili namna ya kukifanya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani ndani na nje ya nchi jana Jijini Dar es Salaam

Katibu Mtendaji Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) Dkt. Selemani Sewangi akitoa taarifa ya namna Kiswahili kinavoendelea kukua wakati wa majadiliano na wadau wa sekta ya Utamaduni kujadili namna ya kukuza na kukifanya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani ndani na nje ya nchi  jana Jijini Dar es Salaam.

Mdau wa Utamaduni Mama Mipango akichangia mada wakati wa majadiliano na wadau wa sekta ya Utamaduni kujadili namna ya kukuza na kukifanya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani ndani na nje ya nchi jana Jijini Dar es Salaam.

: Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye (waliokaa katikati) katika picha ya pamoja na wadau wa sekta ya Utamaduni walipokutana kujadili namna ya kukifanya Kiswahili kuwa bidhaa yenye thamani jana Jijini Dar es Salaam. Wapili kulia waliokaa ni Naibu Waziri wa Habari Mhe. Annastazia Wambura, Wapili kushoto waliokaa ni Katibu Mkuu Wizara ya Habari Prof. Elisante Ole Gabriel, na wakwanza kushoto waliokaa ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari Bibi. Nuru Millao.

Picha na: Genofeva Matemu – WHUSM