SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 24 Agosti 2016

T media news

UKUTA Waipeleka Serikali Kanisani na Misikitini

Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania (UKUTA) uliotangazwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kufanyika kwa maandamano na mikutano ya hadhara Septemba Mosi mwaka huu umeipeleka serikali kanisani kuomba msaada.Anaandika Josephat Isango.

Tayari baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya nchini wamekutana na viongozi wa makanisa kuwaomba waambie waumini wao wasitoke kuandamana na kwenye mikutano ya hadhara ya Chadema.

MwanaHALISI online limefanikiwa kuona barua za kutoka wilaya kadhaa kwenda kwa viongozi wa dini ambazo zilielekeza kufanyika vikao katika ofisi za wilaya kati ya tarehe 22- 23 Agosti 2016 ajenda kuu ikiwa ni kuwashauri viongozi wa dini wawatangazie waumini wao kuwa UKUTA ni sawa na uvunjifu wa amani.

Wakuu wa wilaya hao wamewaonya viongozi wa dini kuwa kama wafuasi wao wataandamana itakuwa ni sawa na viongozi wa dini kushiriki maandamano na mikutano ya hadhara.

Waraka wenye kumb Na.ab.214/433/01 “B” 03 ya Agosti 18 mwaka huu, iliyosainiwa na Kaimu Rozalia J Njiani, Katibu Tawala wa Wilaya ya Karagwe ambayo MwanaHALISI online limeiona ni moja kati ya nyaraka nyingi zilizosambwazwa kwa viongozi wa dini nchini

Viongozi wa dini wameonekana kukasirishwa na uamuzi huo wa serikali lakini baadhi yao wamenukuliwa wakitoa msimamo dhidi ya wito huo wa serikali.

MwanaHALISI online limefanikiwa kuona kiongozi mmoja wa dini akimwandikia mwenzake kuwa “Muda wote tumekuwa kiunganishi kwa vyama vyote. sauti ya kinabii ilibaki pale pale inapotakiwa kuwa hata kama Kanisa lilionekana kuegamia upande mmoja, sheria za nchi ni lazima ziheshimiwe na katiba ya nchi iheshimiwe ndio msimamo wa sisi viongozi wa dini, hatutatetereka.”

Haya yanajiri ikiwa ni muda mchache tangu ofisi ya Msajili wa vyama vya siasa kutangaza kuvikutanisha vyama vyote vilivyojiandaa kufanya maandamano vikutane katika meza ya mazungumzo.

Ukuta ulitangazwa kama azimio la Kamati Kuu ya dharura ya Chadema iliyoketi tarehe 23-26 Julai, 2016 kujadili hali ya siasa na uchumi wa Taifa tangu serikali ya awamu ya tano ilipoingia madarakani mwezi Novemba, 2015.