SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 24 Agosti 2016

T media news

MOURINHO SI RAFIKI WA VIJANA LAKINI ANACHOKIFANYA KINA MAANA ZAIDI

Na Mahmoud Rajab

Kwa kiasi fulani, hii imekuwa ikiihusu klabu ya Manchester United. Ile hali ya furaha na imani kubwa waliyokuwa nayo mashabiki wa United baada ya kumwona Pogba uwanjani huku Zlatan akifanya yake kwenye mchezo dhidi ya Southampton imefunikiwa na huzuni ya kuona wachezaji vijana kutoka kwenye academy yao wakipata huduma isiyostahili kutoka kwa kocha wao Jose Mourinho.

Uamuzi wa Mourinho kutomjumuisha hata kwenye benchi Marcus Rashford kwenye michezo miwili mfululizo tayari umeanza kuwapa mashaka. Tayari amemuuza mchezaji Tyler Blackett kwenda Reading na kumtoa kwa mkopo Cameron Borthwick-Jackson kwenda Wolves, uamuzi ambao umeanza kuwapa United mashaka juu ya mustakabali wa vijana kwenye timu yao.

Kipigo cha timu ya vijana chini ya miaka 23 dhidi ya vijana wenzao wa Southampton kwenye dimba la St Mary kimeleta mshtuko mkubwa, huku wengi wakiuliza ni kwanini wachezaji kama Andreas Pereira, Memphis Depay, Rashford na Will Keane hawakuchezeshwa. Kwamba wachezaji ambao wamekuwa wakipata nafasi kweye kikosi cha wakubwa wanashindwa kupata nafasi kwenye timu ya vijana.

Kwa upande wa Rashford hasa hasa, kukosa nafasi ya kucheza kumeanza kumletea athari, ambapo meneja wa England Sam Allardyce amekiri kwamba haoni sababu ya kumjumuisha kwenye kikosi chake licha ya kuonesha kiwango bora msimu uliopita na kwenye Michuano ya Euro mwaka huu.

“Kwa sasa Rashford hapati muda wa kucheza, hivyo itaniwia vigumu sana kumjumuisha kwenye kikosi changu, maana siwezi kumjaji kwa kiwango cha msimu uliopita ilhali kwa sasa hachezi,” amenukuliwa Allardyce wiki iliyopita akitoa ufafanuzi.

Haya yanakuja wakati awali Mourinho alipotetea rekodi yake dhidi ya wachezaji vijana mwanzoni kabisa wakati alipotambuliwa rasmi kuwa kocha wa Man United. Msimu uliopita Van Gaal aliwapa nafasi vijana kwa kiasi kikubwa hali iyopelekea wengi kuamini vijana hao walikuwa na dalili nzuri za kuwa na mafanikio baadaye. Lakini kwa namna Mourinho alivyofanya usajili wake inaonekana dhahiri ndoto za vijana kupata nafasi kwenye kikosi chake zinazidi kufifia.

Kuondoka kwa mkopo kwa wachezaji Blackett na Borthwick-Jackson, Guillermo Varela, Adnan Januzaj na James Wilson, huku Paddy McNair na Donald Love wakiondoka moja kwa moja, kunawaacha United wakiwa hawana tena vijana wanaoweza kucheza kikosi cha wakubwa ukiwaondoa Jesse Lingard na Rashford. Kwa wachezaji waliobakishwa ambao ni Timothy Fosu-Mensah, Pereira, Keane, Joe Riley, Regan Poole na James Weir hawana nafasi ya ya kucheza kwenye kikosi cha wakubwa na hata hivyo pia wanaweza kutolewa kwa mkopo kabla ya dirisha la usajili kufungwa.

Hali hii inayotekea kwa sasa, si ngeni sana kwani hata Van Gaal alifanya hviyo msimu uliopita baada ya kuwatoa kwa mkopo Januzaj na Blackett pia, lakini aliamua kutoa nafasi ya kucheza japo kwa uchache kwa mchezaji Pereira na baadaye kumjumuisha Rashford na Lingard ambao walionesha uwezo mkubwa kwenye michezo waliyocheza.

Borthwick-Jackson ataongeza uwezo zaidi kwa kupata nafasi kubwa kwenye kikosi cha Wolves kuliko kukaa na kusubiri mpaka Luke Shaw aumie au kushuka kiwango. Pereira atakuwa na nafasi nzuri kwenye kikosi cha Fulham kuliko kubaki klabuni hapo na kusotea benchi.

“Mourinho ameniambia kwamba, ana malengo makubwa na mimi na anaona kuna dalilia nzuri kwa maisha yangu ya baadaye kwenye soka,” Borthwick-Jackson alisema wakati alipokamilisha utaratibu wa kujiunga na Wolves kwa mkopo. “Hivyo kikubwa ninachokiangalia hapa ni kupata uzoefu ili niweze kupata nafasi katika kikosi cha United.”

Kwa wale ambao bado wamebakishwa na Mourinho wanatakiwa kuwa na imani na kocha wao, maana alishawaambia kwamba muda wao wa kucheza utaanza mwezi Septemba kwenye Kombe la Ligi na Europa.

Kwa upande wa Borthwick-Jackson, Januzaj na wengine wanapaswa kujituma na kumridhisha kocha wao ili aweze kuwaamini na kuwarejesha kikosini. Licha ya kuwaondoa moja kwa moja wachezaji McNair na Blackett, lakini naamini United hawatarudia makosa waliyofanya kwa Pogba.

Jambo kubwa zaidi ya yote ni kwamba, United walimhitaji Mourinho ili arejeshe heshima ya United iliyopotea, na ujio wa Pogba na Ibrahimovic umeanza kuleta mwanga wa nini kinaoenda kutokea msimu huu.