SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 6 Aprili 2016

T media news

Hatimaye Utumishi Wafafanua Kuhusu Mshahara wa Rais Magufuli na Kikwete



OFISI ya Rais (Utumishi na Utawala Bora) imefafanua kuhusu mshahara wa Rais John Magufuli ikisema kuwa mishahara ya watumishi wa umma na viongozi wa umma hupangwa katika bajeti, hivyo mshahara wa Rais ni ule ulioidhinishwa katika Bajeti ya mwaka 2015/16.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Dk Laurian Ndumbaro, bajeti ya mishahara yote ya watumishi wa umma na viongozi wa umma hupangwa kila wakati pale bajeti inapoandaliwa na kuidhinishwa na kwamba Rais mpya hakutengenezewa mshahara mpya.

“Wizara yetu ndiyo yenye dhamana ya mishahara ya watumishi wa umma na viongozi wa umma, na hii huandaliwa kila mwanzo wa mwaka kabla ya kuanza kwa mwaka mpya wa fedha. Kwa hiyo mwaka 2015/16 fedha zake ziliidhinishwa Juni mwaka jana na kuanza kutumika Julai,” alisema Dk Ndumbaro.

“Kwa hiyo, bajeti hiyo iliidhinishwa kwa viongozi wote, Rais, Makamu wa Rais, wabunge na watumishi wote wa umma. Hivyo, mshahara wa Rais, kwa mantiki hiyo, Rais Kikwete (Jakaya) ndio huo ambao unatumiwa na Rais John Magufuli. Kama mshahara, hakuna tofauti, hakuna mabadiliko, kiwango ni kile kile. Rais mpya hakutengenezewa mshahara mpya,” alifafanua Katibu Mkuu huyo wa Utumishi na Utawala Bora.

Kumekuwapo na taarifa mbalimbali katika vyombo vya habari  kuhusu mshahara wa Rais na hivi karibuni, baadhi ya vyombo hivyo vilidai kuwa Rais mstaafu Kikwete alikuwa analipwa Sh milioni 34. 

Aidha, Rais Magufuli alikaririwa hivi karibuni akiwa nyumbani kwake Chato mkoani Kagera akisema kuwa analipwa mshahara wa Sh milioni 9.5 na akasema yupo tayari kuonyesha nyaraka zote.