SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Alhamisi, 22 Agosti 2019

T media news

Utangulizi

Katika sehemu ya 1 ya Moduli Utunzaji katika Ujauzito, umejifunza kimsingi kuhusu muundo wa kimaumbile wa mfumo wa uzazi wa mwanadamu na jinsi unavyofanya kazi, awamu za kawaida za ujauzito na mabadiliko ya kuwezesha kubeba mimba, uchunguzi wa kijumla kuhusu jinsi mimba inavyoendelea na jinsi ya kutambua matatizo madogo. Katika sehemu ya 2 ya Moduli yaUtunzaji katika Ujauzito,utajifunza kuhusu kanuni za kimsingi za utunzaji maalum katika ujauzito.
Kipindi hiki kitaanza kwa kueleza dhana na kanuni za utunzaji maalum katika ujauzito na tofauti za kimsingi baina ya huduma hii na mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito. Kipindi hiki kitaangazia vipindi vingine katika sehemu ya 2 ambavyo vyote huwa katika Utunzaji Maalum katika Ujauzito. Pia utajifunza malengo ya kila mojawapo ya ziara nne za utunzaji maalum katika ujauzito. Kipindi hiki kitahitimisha kwa hatua ambazo wewe binafsi na mama mjamzito mnapaswa kutekeleza katika kuzaa; mashauri kuhusu jambo la kufanya iwapo matatizo yataibuka na maelekezo ya jinsi ya kuandika arifa ya rufaa ikiwa mama anapaswa kuhamishwa hadi katika kituo cha afya.

Malengo ya Somo la Kipindi cha 13

Baada ya kuhitimisha kipindi hiki, unatarajiwa:
13.1 Kufasili na kutumia kwa usahihi maneno yote muhimu yaliyoandikwa kwa herufi nzito.(Swali la Kujitathmini 13.1)
13.2 Kujadili kanuni za utunzaji maalumkatika ujauzito na kutaja jinsi unavyotofautiana na mtazamo wa kitamaduni. (Swali la Kujitathmini 13.1)
13.3 Kueleza ratiba, malengo na taratibu zinazofuatwa katika kila mojawapo ya ziara nne za utunzaji maalum katika ujauzito, za wanawake katika kipengele cha kimsingi. (Maswali ya Kujitathmini 13.2 na 13.3)
13.4 Kuwashauri wanawake wajawazito kuhusu maandalizi ya kuzaa pamoja na vifaa watakavyohitaji. (Swali la Kujitathmini 13.4)
13.5 Kutoa muhtasari wa vipengele muhimu vya kujitayarishia matatizo na kupangia matukio ya dharura, ikijumuisha kuwashauri watoaji damu na kuandika arifa ya rufaa. (Swali la Kujitathmini 13.3)

13.1 Dhana na kanuni za utunzaji maalum katika ujauzito

Kihistoria, kielelezo cha kitamaduni cha utunzaji katika ujauzito kilianzishwa miaka ya kwanza ya 1900. Kielelezo hiki huchukulia kuwa ziara za kila mara na kuwaainisha wanawake wajawazito katika viwango vya hatari ya chini na hatari ya juu kwa kutabiri matatizo kabla ya wakati, ndiyo njia mwafaka ya kumtunza mama na fetasi. Utunzaji maalum katika ujauzitoulichukua nafasi ya mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito - huu ni mtazamo wa kimalengo uliopendekezwa na watafiti mnamo mwaka wa 2001 na kuanza kutumiwa na Shirika la Afya Duniani mnamo mwaka wa 2002.
Kusudi la utunzaji maalum katika ujauzito ni kukuza afya ya kina mama na watoto wao kupitia ukaguzi uliolengwa kwa wanawake wajawazito ili kusaidia:
  • Utambuzi na utabibu wa ugonjwa uliothibitishwa
  • Ugunduzi wa mapema kuhusu matatizo na shida zingine zinazoweza kuathiri matokeo ya mimba
  • Proflaksisi na matibabu ya anemia, malaria na magonjwa ya zinaa ikijumuisha VVU, maambukizi ya mfumo wa mkojo na pepopunda. Profilaksisi ni hatua za kuingilia kati zinazolenga kuzuia ugonjwa au matatizo.
Pia, utunzaji maalum katika ujauzito hukusudia kumpa kila mwanamke utunzaji wa kibinafsi ili kudumisha hali ya kawaida ya kuendelea kwa ujauzito kupitia uelekezi na ushauri wa wakati unaofaa kuhusu:
  • Maandalizi ya kuzaa (yalioelezwa baadaye katika kipindi hiki),
  • Lishe, chanjo, usafi wa mwili na upangaji uzazi (Kipindi cha 14)
  • Ushauri kuhusu dalili za hatari zinazoashiria kuwa mwanamke mjamzito anapaswa kupata usaidizi mara moja kutoka kwa mtaalamu wa afya (Kipindi cha 15).
Katika utunzaji maalum katika ujauzito, wahudumu wa afya husisitiza makadirio ya kibinafsi na hatua zinazohitajika ili mhudumu namama mjamzito waweze kufanya uamuzi kuhusu utunzaji katika ujauzito. Hivyo basi, badala ya kufanya ziara za kila mara za kitamaduni za utunzaji katika ujauzito kuwa desturi kwa wote, na kuwaainisha wanawake kwa kuzingatia kiashiria hatari cha kidesturi, wahudumu wa utunzaji maalum katika ujauzito huongozwa na hali ya kibinafsi ya mwanamke.
Mtazamo huu pia hufanya utunzaji katika ujauzito kuwa jukumu la familia. Mhudumu wa afya hujadili na mwanamke na mumewe kuhusu matatizo ambayo mama anaweza kukumbana nayo; pamoja wanapanga kujitayarishia kuzaa na kujadili utunzaji wa baada ya kuzaa pamoja na maswala ya uzazi wa baadaye. Wanawake wajawazito hupata utunzaji wa asili wakiwa nyumbani na katika kituo cha afya; familia pamoja na wahudumu wa afya hutambua matatizo mapema; na hatua za kuingilia kati huanzishwa kwa wakati unaofaa hivyo kuwa na matokeo bora zaidi kwa akina mama na watoto wao.
Kisanduku 13.1 kinatoa muhtasari wa kanuni za kimsingi za utunzaji maalum katika ujauzito.

Kisanduku 13.1 Kanuni za kimsingi kuhusu utunzaji maalum katika ujauzito

  • Wahudumu wa utunzaji katika ujauzito hufanya utathmini mkamilifu wa mwanamke mjamzito ili kutambua na kutibu matatizo yaliyoko ya kiukunga na kitabibu.
  • Wao huendesha proflaksisi kama ilivyoashiriwa, kama vile hatua za kuzuia malaria, anemia, upungufu wa lishe, magonjwa ya zinaa ikijumuisha kuzuia kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi kwa mtoto (tazama Kipindi cha 16), na pepopunda.
  • Wakiwajumuisha kina mama, wahudumu hawa huamua mahali pa kufanyia ziara fuatilizi za utunzaji katika ujauzito, jinsi ziara hizo zitakavyofuatana, mahali pa kuzalishia na atakayehusika katika utunzaji wa ujauzito na wa baada ya kuzaa.
  • Mradi tu kiwango cha utunzaji kimetiliwa mkazo katika kila ziara na wachumba wanafahamu hatari zinazoweza kutokea wakati wa ujauzito, mimba nyingi huendelea bila matatizo.
  • Hata hivyo hakuna ujauzito unaoweza kuwa 'bila hatari' hadi udhibitishwe, kwa sababu matatizo yanayohusiana na ujauzito, yakiwemo yenye athari mbaya na yasiyo na athari mbaya huwa hayatabiriki pamoja na matukio ya awamu za mwisho ya ujauzito.
  • Mwanawake mjamzito na mumewe huaminika kuwa 'wagunduzi wa hatari' baada ya kupata ushauri kuhusu dalili za hatari na pia 'washiriki' wa huduma ya afya kwa kukubali na kutekeleza mapendekezo yako.

13.1.1 Manufaa ya utunzaji maalum katika ujauzito

Utunzaji maalum katika ujauzito umepata umaarufu kwa sababu ya manufaa yake katika kupunguza vifo vya kina mama na uwezo wa kufa na maradhi(ugonjwa, matatizo au ulemavu) ya kipindi kinachokaribiana na kuzaliwa. Uwezo wa kufa katika kipindi kinachokaribiana na kuzaliwani idadi ya jumla ya uzazimfu(watoto wanaozaliwa wafu baada ya wiki 28 za ujauzito) ikijumlishwa na idadi ya jumla ya watoto wachanga (watoto wazawa) ambao hufariki katika siku 7 za kwanza za maisha. Kima cha vifo katika kipindi kinachokaribiana na kuzaliwani idadi ya watoto wanaozaliwa wafu na vifo vya watoto wachanga vinavyotokea kwa kila watoto 1000 waliozaliwa hai, na ni kipimo kilichotambulika ulimwenguni kote cha kiwango cha utunzaji katika ujauzito.
  • Ufasili wa uwiano wa kiwango cha vifo vya kina mama ni upi? (Ulijifunza haya katika Kipindi cha 1 cha Moduli hii.)
Utunzaji katika maalum ujauzito ni mtazamo mwafaka kwa nchi zisizo na raslimali za kutosha ambapo wataalamu wa afya ni wachache na miundo msingi ya afya ni duni. Hususani, wanawake wengi wajawazito hawawezi kukimu gharama ya ziara za kila mara kama inavyohitajika katika mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito. Katika mtazamo wa kimipango na kifedha, mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito hauwezi kutekelezwa katika wanawake wengi wajawazito na ni mzigo kwa mfumo wa afya. Kwa hivyo, mataifa mengi yanayoendelea yanachukua mtazamo wa utunzaji maalum katika ujauzito.

13.1.2 Kasoro za mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito

Utafiti (kwa mfano, tazama Kisanduku13.2) umeonyesha kuwa ziara za kila mara za kipindi cha ujauzito kama ilivyo katika mtazamo wa kitamaduni haziboreshi matokeo ya ujauzito. Hususan, wanawake wajawazito unaoitajika kuwa na 'hatari ya chini' au 'wasio na hatari' katika mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito huenda wasipate ushauri kuhusu dalili za hatari. Hivyo, mara nyingi wanawake hawa hawatambui dalili za hatari hivyo hawawaarifu wataalamu wa afya haraka iwezekanavyo.
Kisanduku 13.2 Kukosa kutambua mimba 'zilizo hatarini'
Kwa kuchukua kutokea kwa leba iliyokwama kama mojawapo ya kiashiria, utafiti wa mwaka wa 1984 nchini Zaire katika wanawake 3,614 wajawazito ulionyesha kuwa asilimia 71 ya wanawake walio na leba iliyokwama walikuwa wameainishwa kama 'wasio na hatari' hapo awali, wakati asilimia 90 ya wanawake waliogunduliwa kuwa 'katika hatari' hawakupata leba iliyokwama. Hii ni asili moja ya ushahidi kuonyesha kuwa matatizo mengi ya ujauzito hayawezi kutabirika na hutokea katika awamu za mwisho.
Mifano mingine ya matatizo ya ujauzito yasiyoweza kutabirika ambayo hutokea katika awamu za mwisho zaidi za ujauzito hujumuisha visababishi vitatu vikuu vya vifo vingi vya kina mama:
  • Matatizo ya hipatensheni katika ujauzito(hipatensheni humaanisha shinikizo la juu la damu hasa eklampsia, ambayo kwa kawaida hutokea katika ujauzito awamu za mwisho za ujauzito, wakati wa leba au baada ya kuzaa (utajifunza haya katika Kipindi cha 19).
  • Kuvuja damu (kuvuja damu nyingi) kwa kawaida hutokea katika trimesta ya tatu (Kipindi cha 21 kinaeleza kuvuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito) au hasa hali hatari ya kuvuja damu baada ya kuzaa, ambayo hutokea baada ya kuzaa (utajifunza haya katika Moduli ya Utunzaji wa Leba na Kuzaa).
  • Maambukizi yanayohusiana na ujauzito (Maambukizi ya uterasi baada ya kuzaa) ambayo kwa kawaida hutokea baada ya kuzaa (kama ilivyoelezwa katika Moduli ya Utunzaji wa Leba na Kuzaa).
Mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito umeshindwa kutambua kwa hakika wanawake walio ’katika hatari' ya kupata hali hizi zinazotishia maisha. Mtazamo huu hutambua baadhi ya wanawake kama walio na 'hatari ya chini' ambao baadaye hupata dalili za hatari zinazohitaji wataalamu kuingilia kati kwa dharura.

13.1.3 Ulinganishaji wa utunzaji katika ujauzito wa kitamaduni na utunzaji maalum

Jedwali 13.1 kinatoa muhtasari wa tofauti za kimsingi baina ya mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito na utunzaji maalum
Matumizi ya dawa za kulevya hujumuisha tumbaku, vileo, miraa, dawa zilizopigwa marufuku, bangi, kokeini na dawa nyinginezo