SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Ijumaa, 8 Septemba 2017

T media news

Donald Trump Alaani Shambulio la Risasi la Tundu Lissu

SERIKALI ya Marekani inayoongozwa na Rais Trump kupitia ubalozi wake ulioko hapa nchini, imeeleza kusikitishwa na tukio la kushambuliwa kwa risasi Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu.
“Marekani imesikitishwa sana kuhusu kupigwa risasi kwa Tundu Lissu, Mbunge na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika. Tunalaani kitendo hiki cha kipuuzi na cha kutumia nguvu. Tunaungana na Watanzania kutoa matumaini yetu ya dhati ili apone haraka.
———————————
The United States is deeply saddened by the shooting of Tundu Lissu, Member of Parliament and President of the Tanganyika Law Society. We condemn this senseless act of violence and join Tanzanians in expressing our sincere hopes for his full and speedy recovery.” Imesema taarifa ya Ubalozi wa Marekani nchini iliyotolewa kupitia ukurasa wake wa Facebook.

Ubalozi huo umesema unaungana na Watanzania katika kumtakia kheri Lissu ambaye pia ni Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) ili apone haraka.

Lissu jana Alhamisi saa sita usiku alisafirishwa kwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan iliyopo Nairobi, Kenya.
Awali, alipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Dodoma baada ya kushambuliwa. Spika wa Bunge, Job Ndugai amesema leo Ijumaa asubuhi kuwa, Lissu alishambuliwa kwa risasi kati ya 28 hadi 32, huku tano zikimpata mwilini.
 Akitoa taarifa ya tukio hilo kwenye kikao cha Bunge, Ndugai amesema risasi mbili zilimpata Lissu kwenye miguu, mbili tumboni na moja kwenye mkono.
Aidha, Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Vincent Mashinji amesema kuwa amepokea taarifa kutoka kwa Mwenyekiti  wa Chama hicho, Freeman Mbowe kuwa Tundu Lissu amezinduka leo asubuhi akiwa katika Hospitali ya Aga-Khan jijini Nairobi nchini Kenya,  kwa sasa ameshazinduka anajitambua na anaendelea vizuri.