SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 8 Machi 2017

T media news

Wabunge wa Burundi wasusia vikao Bunge la Afrika Mashariki


Wawakilishi watano wa bunge la Afrika mashariki EALA kutoka Burundi wamesusia kuhudhuria kikao cha bunge hilo mjini Kigali wakihofia usalama wao.

Bunge hilo la EALA litafanya vikao vyake nchini Rwanda kutoka tarehe 6 had 17 mwezi Machi 2017.

Ni vikao vya mwisho kabla ya wanachama wapya kuteuliwa mnamo tarehe 5 mwezi Juni 2017.

Kabla ya vikao hivyo kuanza siku ya Jumanne ,wabunge watano kati ya tisa wanaowakilisha Burundi katika vikao hivyo vya EALA walimwambia Spika Daniel Fred Kidega kwamba hawawezi kuhudhuria vikao hivyo nchini Rwanda kutokana na maswala ya kiusalama.

Huku rais Paul Kagame akifungua rasmi vikao hivyo, ni wabunge wanne pekee kutoka Burundi waliohudhuria.

Katika mkutano na vyombo vya habari Spika wa EALA Daniel Fred Kidega alisema kuwa kutokuwepo kwa wabunge hao wa Burundi hakutaathiri vikao hivyo.

''Sio mara ya kwanza kwamba nimepokea malalamishi hayo ya kiusalama, lakini tuna njia za kutatua hali ili kuwa ya kawaida'', aliongezea.

Kidega alielezea kwamba Rwanda ilimuhakikishia usalama wa kutosha licha ya wasiwasi wa raia hao wa Burundi.