SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 8 Machi 2017

T media news

Thomas Ulimwengu Apewa Mazoezi Ya Ziada Ulaya


MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Thomas Ulimwengu amesema kwamba amekuwa anapewa mazoezi ya ziada katika klabu yake mpya, AFC Eskilstuna ya Sweden ili awe fiti zaidi, kwa sababu alijiunga na timu hiyo akitoka kuuguza maumivu ya mguu.

Akizungumza  Online leo, Ulimwengu amesema kwamba alijiunga na AFC Eskilstuna baada ya kuwa nje kwa takriban miezi mitatu kutokana na maumivu ya mguu.

“Ninapewa mazoezi ya ziada hapa kwa sababu nilikuja katika hii timu baada ya kuwa nje kwa miezi kama mitatu kwa sababu ya maumivu ya mguu. Hivyo sikuwa fiti kiasi cha kutosha,”amesema.

Ulimwengu amesema kabla ya mazoezi ya pamoja na wenzake, amekuwa akifanyishwa mazoezi maalum ya kumuweka fiti zaidi na kwa ujumla anaendelea vizuri. 

Ulimwengu alijiunga na Eskilstuna ambayo awali ilikuwa inajulikana kama FC Cafe Opera na Vasby United Januari mwaka huu kwa mkataba wa miaka miwili akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Ulimwengu aliyezaliwa Juni 14, mwaka 1993 aliibukia katika taasisi ya soka Tanzania (TSA) mwaka 2008, kabla ya mwaka 2009 kwenda kuanza kukomazwa Ligi Kuu katika klabu ya Moro United alikokuwa akicheza kwa mkopo hadi mwaka 2010 alipokwenda akademi ya AFC Eskilstuna ya Sweden, alikocheza hadi 2011 TP Mazembe alipochukuliwa na timu ya vijana ya Mazembe.

Alicheza U-20 ya Mazembe kwa msimu moja kabla ya kupandishwa rasmi timu ya wakubwa mwaka 2012 na moja kwa moja kuwa mchezaji wa kikosi cha kwanza hadi anamaliza Mkataba wake Oktoba mwaka jana.

Ulimwengu anajivunia kushinda mataji makubwa akiwa na  Mazembe kama Ligi ya Mabingwa Afrika, Super Cup ya Afrika na pamoja na kucheza Klabu Bingwa ya Dunia.

Ulimwengu tayari ameanza kuichezea timu yake mpya nchini Sweden