SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 8 Machi 2017

T media news

CUF ya Maalim Seif (Mtatiro) Yamjibu Prof. Lipumba Juu ya Kumsimamisha Kazi Katibu Mkuu...!!


Nimeulizwa na watu wengi sana kuhusu tamko la jana la Lipumba (BWANA YULE) la kuwavua ukurugenzi wakurugenzi wote wa CUF Zanzibar na kumteua Sakaya kuwa Katibu Mkuu. Nachoweza kuwaeleza ni kuwa; “kichaa akiiba nguo zako, usikimbizane naye ukiwa hujajisitiri, kavae nguo kwanza”. Wenye akili na waelewe!

Ukweli ni kuwa Katibu Mkuu wa CUF anachaguliwa na Mkutano Mkuu wa CUF, kamwe hawezi kuteuliwa na Mwenyekiti wa CUF (hata kama Lipumba angelikuwa ndiye mwenyekiti wa CUF kama ilivyokuwa zamani). 

Pili, wakurugenzi wa CUF wanateuliwa na Mwenyekiti wa CUF kwa kushauriana na Makamu Mwenyekiti wa CUF. Mwenyekiti wa CUF alijiuzulu tokea mwaka 2015 na Mkutano Mkuu wa taifa uliidhinisha kujiuzulu kwake tarehe 21 Agosti 2016, kwa hiyo CUF haina Mwenyekiti kwa sasa. Yupo mhuni mmoja tu amekalia ofisi na anaishi ofisini kwa kulindwa na dola! 

Makamu Mwenyekiti wa CUF alijiuzulu na kujiunga CHADEMA kwa maslahi ya kitaifa kwenye uchaguzi mkuu na hajachaguliwa mtu mwingine kushika wadhifa huo. 

Kama kuna mtu anasimama hadharani na kufukuza wakurugenzi wa CUF Bara au Zanzibar hivi sasa, basi mtu huyo si Mwenyekiti wa CUF, labda ni MSUKULE wa mwenyekiti wa CUF. Itoshe tu kusema kuwa Lipumba anatumiwa vibaya sana na kama kuna wanasiasa wanatumika basi kwa sasa yeye ana PhD ya eneo hilo. 

Lakini nataka kuwahakikishia watanzania kuwa katika CUF tuko imara sana, Kamati ya Utendaji ya Taifa inayotambulika ndani ya chama na iliyothibitishwa na Baraza Kuu ipo na inakutana kila mara, kwa hiyo kikatiba huwezi kuwa na Kamati nyingine ya utendaji ya taifa isipokuwa ili iliyothibitishwa na Baraza Kuu ambalo wajumbe wake huchaguliwa na Mkutano Mkuu. 

Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la CUF lipo na linakutana kama kawaida. Bodi ya Wadhamini ya CUF ipo na imefanya maamuzi mengi hivi karibuni, ikiwa ni pamoja na kuzifunga akaunti zote za CUF ili zisiendelee kutumiwa na Bwana Yule kutorosha fedha za chama na kugawana na genge lake n.k. 

Kama nilivyowahi kusema huko nyuma na narudia tena hapa, jeuri yote ya Lipumba ni CCM na serikali yake, hawa ndio wanamuweka mjini, anatamba, anaita vyombo vya habari, anatangaza madudu yake n.k. 

Lakini kitaalamu tumeshamshinda vita ya ndani, bado ameshikilia tawi moja tu, CCM na vyombo vya dola – nawahakikishia kuwa tawi hilo litakatika na Lipumba ataanguka kama mzigo na genge la wahuni wake litatawanyika kama kondoo wasio na mfugaji na CUF imara itasimama kuelekea 2020.

Kwa hiyo msitishwe na matamko ya Lipumba na watu wake, ni kweli watatusumbua sana, lakini tutawashinda tu, na mahali tutakapowashindia wanapajua na hawana pa kutokea. Hakuna UONGO iliyowahi kuishinda KWELI. 

Hakuna WASALITI waliowahi kudumu kwa hiyo nawaomba watanzania tuendelee kumpuuza kama wanachama wa CUF mkoani Tanga walivyompuuza hivi karibuni alivyojaribu kufanya ziara mkoani humo. Tumkatae kama wabunge na madiwani wa CUF walivyomkataa. Tumsuse kama wenyeviti wa mitaa wa CUF walivyomsusa. 

Tuendelee kumzodoa kama anavyozodolewa na familia yake. Let us disown and continue to neglect him untill CCM registers him officially.

Julius Mtatiro,

Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi,

The Civic United Front,

07 Machi 2017.