SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Alhamisi, 3 Novemba 2016

T media news

Nyota ya Bulaya Chadema kama mbalamwezi

Dodoma. Nyota ya siasa ya Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya imeendelea kung’ara vizuri ndani ya Chadema baada ya juzi kuwabwaga wabunge wakongwe katika uchaguzi wa kupata wabunge watano wa kuwakilisha katika Kamati Kuu.

Uchaguzi huo uliitishwa kwa mujibu wa Ibara ya 7.7.14 (g) ya Katiba ya Chadema inayotoa nafasi ya wabunge watano kuchaguliwa kwa ajili ya kuwakilisha wenzao kwenye Kamati Kuu ya chama.

Wabunge 20 walijitokeza kuwania nafasi hizo, baadaye wanane walijitoa wakabaki 12 ambao baada ya kupigiwa kura, Bulaya ambaye alijiunga na Chadema Agosti mwaka jana, alifanikiwa kuwabwaga wazoefu ndani ya chama hicho.

Msimamizi wa uchaguzi huo, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Vicent Mashinji aliwatangaza wabunge watano na kura zao katika mabano kuwa ni Bulaya (47), Godbles Lema (41), Tundu Lissu (40), Joseph Mbilinyi (37) na Mariam Msabaha (30).