SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 6 Aprili 2016

T media news

UFAFANUZI WA MSHAHARA WA RAIS KIKATIBA


                           


Siku chache baada ya Rais Dk. John Magufuli, kutaja mshahara wake kuwa ni Sh. milioni 9.5 kwa mwezi, Wizara ya Ofisi ya Rais, Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, imefafanua mshahara aliokuwa anapokea Rais wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete, kuwa unalingana na wa kiongozi huyo.

Katibu Mkuu Utumishi, Dk. Laurean Ndumbaro  alisema Kikwete aliondoka madarakani akiwa anapokea Sh. milioni 9.5, ikiwa ni kiwango sawa na cha Rais Magufuli.

Rais alilazimika kufanya hivyo kufuatia Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema) na Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT-Wazalendo), kumpa changamoto ya kutaja mshahara wake, baada ya kueleza nia ya serikali yake kupunguza mishahara ya watumishi wa mashirika na taasisi zake kutoka Sh. milioni 40 hadi milioni 15.

Iwapo Rais mstaafu Kikwete, alikuwa analipwa kiasi hicho, kwa mujibu wa sheria, kwa sasa analipwa asilimia 80 ya mshahara huo ambayo ni Sh. milioni 7.6 ya mshahara wa Rais aliyeko madarakani.

Hivi karibuni, baadhi ya vyombo vya habari vilinukuu taarifa iliyotolewa Julai, mwaka jana na mtandao wa Africa Review ulioandika kuwa Rais Kikwete wakati akiwa madarakani alikuwa akishika nafasi ya tano miongoni mwa marais 38 wa Afrika kwa kulipwa mshahara mnono wa Dola 16,000 za Marekani (sawa na Sh. milioni 34 wakati huo).

Taarifa hizo zilikanushwa vikali na Ikulu, lakini hakukuwa na ufafanuzi wa mshahara halisi anaopokea Rais kwa wakati huo.

Kwa mujibu wa Katiba ibara ya 43 (1), Rais atalipwa mshahara na malipo mengineyo na atakapostaafu, atapokea malipo ya uzeeni, kiinua mgongo, posho, kadiri itakavyoamuliwa na Bunge na mshahara, malipo hayo mengineyo, malipo ya uzeeni na kiinua mgongo hicho, vyote vitatokana na Mfuko Mkuu wa Hazina ya serikali na vitatolewa kwa mujibu wa masharti ya ibara hiyo.

Ibara ndogo ya pili inasema mshahara na malipo mengineyo yote ya Rais havitapunguzwa wakati Rais atakapokuwa bado ameshika madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba. KATIBA YA JAMURI YA MUNGANO WA TANZANIA