SASA UNAWEZA DOWNLOAD T MEDIA NEWS APPS.

Jumatano, 8 Machi 2017

T media news

Katibu wa Chadema Simanjiro Ang'atuka


Katibu wa Chadema Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, Frank Oleleshwa ameandika barua ya kujiuzulu nafasi hiyo na kuzua taharuki kwa baadhi ya wanachama na viongozi wa eneo hilo.

Akizungumza  leo Oleleshwa alisema ameamua kwa hiyari yake kuachia nafasi hiyo aliyoishikilia kwa zaidi ya miaka minne sasa kwa dhamira safi na moyo mweupe, hivyo anampisha katibu mwingine.

Amesema alijiunga na Chadema Mei, 2012 akiwa anasoma chuo cha wanyamapori Mwika mkoani Kilimanjaro na kisha akaanza harakati za kukijenga chama hicho jimbo la Simanjiro.

Alisema japo wapo watakaobeza jitihada na juhudi zake, lakini ameshiriki kufanikisha ushindi wa Chadema kwa kupata mbunge, madiwani wa kata sita na baadhi ya wenyeviti wa vijiji na vitongoji.

Alisema kujiuzulu kwake haina maana kuwa ameenda likizo ya kutofanya kazi ya Chadema jimbo la Simanjiro, kwani bado ana wajibu kama mwanachama kwa kuilinda, kuitetea na kuijenga.